Magufuli atoa onyo la mwisho

MAGUFULI AKERWA NA MICHANGO MASHULENI

Muktasari:

Alisema Serikali inatoa Sh23.8 bilioni kila mwezi kwa ajili ya kuwezesha utoaji wa elimu bila malipo, lakini anashangaa kuona bado kuna walimu wanaendelea kuwatoza michango ama kuwarudisha nyumbani wanafunzi wanaoshindwa kutoa michango hiyo.

Dar es Salaam. Takriban wiki moja iliyopita, Rais John Magufuli alieleza jinsi baadhi ya wateule wake wasivyomuelewa anataka nini, na jana alionekana kutoa hisia kama hizo baada ya wazazi kuendelea kulalamikia michango licha ya kuwepo elimu bure.

Magufuli aliamua kutekeleza ilani ya CCM ya kutoa elimu bure kuanzia elimu ya msingi hadi sekondari kuanzia mwaka jana akisisitiza wakuu wa shule kutoendesha michango yoyote, lakini katika siku za karibuni kumekuwepo na malalamiko ya wazazi kuchangishwa fedha kwa ajili ya malengo tofauti.

Jana, Rais Magufuli alikutana na Profesa Joyce Ndalichako, ambaye ni Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Seleman Jafo (Waziri wa Nchi, Tamisemi) na kuzungumzia suala hilo.

“Kwa taarifa hii mkawaeleze wakuu wa mikoa, wilaya na wakurugenzi. Nikisikia kuna shule katika wilaya fulani ambayo watoto wanarudishwa kwa sababu hawajachangia kitu fulani, huyo mkurugenzi (wa wilaya) ajihesabu hana kazi,” alisema Rais Magufuli.

Aliwataka mawaziri hao, wakurugenzi wa halmashauri na walimu kuhakikisha hakuna mwanafunzi wa shule ya msingi na sekondari atakayefukuzwa shuleni kwa sababu ya kutolipa michango.

Alisema Serikali inatoa Sh23.8 bilioni kila mwezi kwa ajili ya kuwezesha utoaji wa elimu bila malipo, lakini anashangaa kuona bado kuna walimu wanaendelea kuwatoza michango ama kuwarudisha nyumbani wanafunzi wanaoshindwa kutoa michango hiyo.

“Nilisema elimu bure na haiwezi kuja kwa mgongo mwingine ikawa elimu pesa. Tumeweka utaratibu kwamba kuanzia shule ya msingi hadi sekondari hakuna kulipa ada yoyote, lakini sasa hivi michango ni ya kila aina,” alisema Rais Magufuli.

Alisema hata walimu hawaruhusiwi kushika michango kutoka kwa wanafunzi.

“Na walimu wote, popote walipo wasishike mchango wowote wa mwanafunzi. Uwe wa maabara, uwe wa madawati, uwe wa nani, wasishike mchango wowote kutoka kwa mwanafunzi,” alisema.

“Michango kama ipo, kama kuna mzazi ana interest ya kuchangia, atapeleka kwa mkurugenzi. Mkurugenzi yule kama atataka kutengeneza madawati, atatengeneza na kupeleka shule husika husika, lakini si mwanafunzi arudishwe kwa sababu hakutoa mchango wa dawati.”

Januari 8, Rais alieleza kutoridhishwa na utendaji wa Wizara ya Madini, ambayo ilishindwa kusaini Kanuni za Sheria ya Madini kwa takriban miezi saba, na Wizara ya Kilimo, Chakula na Umwagiliaji, iliyoshindwa kupeleka mbolea mikoani kwa wakati.

Ilikuwa ni siku chache baada ya kuonyesha kutoridhishwa na utendaji wa Wizara ya Fedha na Mipango, Wizara ya Mambo ya Ndani na Wizara ya Mawasiliano na Uchukuzi kwa kushindwa kushughulikia magari yaliyokaa bandarini kwa zaidi ya miaka miwili.

Baadhi ya wadau wa elimu wamekuwa wakiuelezea mpango wa elimu bure kuwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo kutofikishwa kwa ruzuku katika baadhi ya shule.

Hivi karibuni wakati akihojiwa na televisheni ya Azam, Waziri Mkuu wa zamani, Frederick Sumaye na mchambuzi wa siasa, Edga Mwandamane alisema kuna mkanganyiko wa ufahamu wa elimu bure na elimu bila malipo na kuwataka viongozi wa Serikali kufafanua jambo hilo.

Alisema licha ya ada kuondolewa, kumekuwa na michango mingi inayozidi hadi ada na hivyo kuwa kero kwa wazazi.

Lakini jana, Rais Magufuli alisema kuanzia sasa marufuku wanafunzi kutozwa michango hiyo.

“Michango sitaki kusikia. Sitaki kusikia mwananchi mahali popote akilalamika kwamba mtoto wake amerudishwa shule kwa sababu ya mchango,” alisema.

Alisema ikitokea katika wilaya mwanafunzi akarejeshwa nyumbani kwa kushindwa kulipa michango, mkurugenzi wa wilaya husika atafukuzwa kazi.

“Hii waanze kutekeleza kuanzia leo. Maofisa elimu wote wakasimamie hili. Haiwezekani tukawa tunatoa elimu bure halafu tutengeneze kero kwa watoto wanaosoma,” alisema.

Alisema wanafunzi kuongezeka ni changamoto ambazo Serikali lazima izibebe na kutaka zisitumike kama kisingizio cha kuwazuia wanafunzi kwenda shule.

“Wapo watoto walioacha kwenda shule kwa sababu ya michango hii,” alisema.

Kwa upande wake, Profesa Ndalichako alituma salamu wa watendaji mbalimbali, akiwataka wahakikishe wanafunzi waliorejeshwa nyumbani kwa sababu ya kukosa mchango, wanarudishwa shule mara moja.

“Kama kuna michango ambayo imechukuliwa kinyume na taratibu wazazi warejeshwe michango. Michango inayotakiwa ni ile ya hiari. Wananchi wanahimizwa kushiriki katika shughuli za maendeleo kwa hiari yao wenyewe kama ambavyo tunachangia maharusi,” alisema Profesa Ndalichako.

Alisema haitakiwi michango kuwa kero.

“Hivi vikwazo vya watoto kupata elimu vimefutwa. Wizara yangu ndio inasimamia Sera ya Elimu. Naomba tusiwe na watu wengine tofauti na wizara ambayo imepewa dhamana ya kusimamia elimu,” alisema na kutaka miongozo ya wizara kuheshimiwa.

Kwa upande wake, Jafo alisema ana taarifa kuwa baadhi ya walimu hutumia fedha hizo za michango kwa ajili ya kujikimu.

“Tumepata taarifa kutoka Halmashauri ya Songea. Kuanzia leo (jana) hii tutaanza kufanya uhakiki maeneo mbalimbali. Itakapobainika ndani ya wiki hii tutaanza kuwachukulia hatua wale walioshiriki katika jambo hili,” alisema.

Aliwataka wakuu wa mikoa na wilaya nchini mpaka kufikia kesho wawasilishe taarifa ofisini kwake kuhusu baadhi ya shule zinazokiuka utaratibu wa Serikali ili waanze kuwachukulia hatua walimu wakuu na maofisa elimu wa halmashauri.

“Hatuwezi kuvumilia lifanyike jambo ambalo limeshatolewa muongozo na watu wanaendelea kufanya kinyume. Tunataka wananchi wanyonge wapate huduma kama Rais alivyoagiza,” alisema.

Jijini Arusha agizo la Rais limepokewa kwa hisia tofauti katika shule kadhaa za msingi na Sekondari, ikielezwa kuwa kumekuwa na michango ya chakula, mlinzi, choo na maji ambayo ni zaidi ya Sh50,000 kwa mtoto mmoja.

Mzazi mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Juliana Laizer alisema mtoto wake ametakiwa kuchanga Sh47,000 mbali na fedha za chakula.

“Kuna mchango wa ukuta wa shule. Kila mtoto Sh 25,000 pia kuna mchango wa mlinzi, choo na maji ambayo ni Sh 27,000,” alisema.

Alisema mbali na mchango huo, kila Jumamosi mtoto anatakwa kwenda shuleni na Sh1,500 kwa ajili ya masomo ya ziada.

Katika shule kadhaa wilayani Arumeru, wazazi wametakiwa kuwapeleka shule  watoto  wakiwa na debe moja na nusu la mahindi, sadolini nne za maharage na Sh5,000 kwa kila mtoto.

“Kupitia kikao cha wazazi tulikubaliana kutoa mahindi na maharage  kwa ajili ya chakula na mambo mengine sasa imekuwa ngumu sana kupata,” alisema Lomayani Mollel.

Hata hivyo, baadhi ya walimu katika shule hizo kwa sharti la kutotajwa majina walisema michango hiyo imekubaliwa na wazazi kupitia vikao vyao ili kuhakikisha watoto wanapata chakula shuleni.

“Waraka wa elimu wa mwaka 2015 unasema wazi jukumu la chakula shuleni ni la mzazi hivyo, wamekuwa wakichanga chakula na fedha kidogo za kuni,” alisema mmoja wa walimu hao.

Katika Manispaa ya Tabora, wazazi wa wanafunzi katika baadhi ya shule za sekondari wamelalamikia kulazimishwa kuchangia Sh10, 000 za chakula.

Mzazi mmoja, Mohamed Musa alisema kiwango hicho ni kikubwa kulinganisha na Sh20,000 ya ada kwa mwaka iliyofutwa na Serikali tangu Januari 2016.

“Tulikuwa tunalipa ada ya Sh20,000 kwa mwaka kwa shule za kutwa ambayo Serikali iliifuta katika mpango wa sera ya elimu bure ya msingi,” alisema.

“Kutakiwa kulipa Sh10,000 kwa mwezi kwa miezi kumi ya masomo ni sawa na Sh100,000 kwa mwaka ambayo ni kubwa kulinganisha na ada iliyofutwa.”