Majadiliano ya makinikia yanaendelea

Muktasari:

  • Majadiliano yanaendelea na wananchi wataelezwa kitakachojiri.
  • TRA imeitaka Kampuni ya Acacia kuilipa Serikali ya Tanzania Dola za Marekani Bilioni 190 ambazo ni zaidi ya Sh 434 trilioni

Dar es Salaam. Wakati majadiliano kati ya Serikali ya Tanzania na Kampuni ya Barrick Gold Corporation kuhusu wizi unaodaiwa kufanywa kwenye uchimbaji na usafirishaji wa mchanga wa madini (makinikia) yakiingia siku ya 64, Ikulu imesema majadiliano hayo yanaendelea.

Majadiliano hayo yanafanyika kipindi ambacho Watanzania wengi wana shauku ya kuona rasilimali za madini zinanufaisha Taifa.

Katika majadiliano hayo yaliyoanza Julai 31, timu ya Tanzania inaongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi.

Akizungumza na Mwananchi leo Jumatatu, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais- Ikulu, Gerson Msigwa amesema majadiliano yanaendelea na wananchi wasubiri wataelezwa kitakachojiri.

“Majadiliano bado yanaendelea, wakiwa tayari watasema kwani hawawezi kuwa wanajadiliana mara wanakwenda kusema katika media," amesema Msigwa.

 

Mazungumzo hayo yalianza kufanyika kipindi ambacho Rais John Magufuli alikuwa amekwishapiga marufuku ya kusafirisha nje makinikia hadi mgogoro wa kimaslahi kati ya wawekezaji hao na Serikali utakapomalizika.

Miongoni mwa kinachojadiliwa ni kodi ambayo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeitaka Kampuni ya Acacia kuilipa Serikali ya Tanzania Dola za Marekani Bilioni 190 ambazo ni zaidi ya Sh 434 trilioni zinazodaiwa kutokana na malimbikizo ya kodi na adhabu.

 

Msingi wa mazungumzo hayo ni baada ya Rais Magufuli kuunda tume mbili kuchunguza madai ya wizi na ufisadi unaodaiwa kufanywa na wawekezaji hao kwa zaidi ya miaka 19 iliyopita tangu walipoanza uzalishaji wa dhahabu.