Linah Sanga si msanii ni mwimbaji hasa-Amini

Msanii wa muziki wa kizazi kipya Amini Mwinyimkuu amesema kuwa wana mpango wa kutoa albamu moja yenye nyimbo 10 na Linah Sanga.

Hivi karibuni Amini na Linah waliachia wimbo wao wa pamoja uitwao ‘Nimenasa’.

Amini amezitaja sababu za kufanya wimbo huo na Linah kuwa ni mwimbaji na si msanii mjanja mjanja.

“Tuliisubiri hii kolabo kwa miaka tisa, tangu tulipotoa ‘Umutima’ mwaka 2010.

“Mashabiki walikuwa wakituulizia sana tunashukuru ‘Nimenasa’ wameipokea vizuri licha ya kuwa tulitanguliza audio,” amesema Amini.

Akizungumzia wapenzi wao walikuwa wanachukuliaje picha za matangazo ya wimbo wao alisema “Hamna namna kwa sababu wapenzi wetu wametukuta kwenye kazi ya muziki lazima wavumilie na watambue kuwa kwetu muziki ni kazi na tunaweza kufanya na mtu yeyote ili kutimiza lengo la kuwapa ladha mashabiki.

Amini ambaye ameachia wimbo mwingine unaokwenda kwa jina la ‘Sina Noma’, amesema kwamba pamoja na wapenzi wao kuwaelewa pia walilazimika mara kadhaa kufanya mawasiliano ya faragha kwa kuogopa kuharibu uhusiano wao.

“Kama binadamu lazima awe na wivu pale anapokuona unawasiliana na mpenzi wako wa zamani ambaye mlipendana sana, hivyo haikuwa rahisi kuwasiliana mbele yao, lakini nashukuru kwa sababu kila kitu kilikwenda sawa,” amesema.