Maswali magumu matano kwenye usaili wa kazi na jinsi ya kujibu

Muktasari:

  • Chukua tahadhari. Majibu haya si msahafu bali mifano tu ya kukupa mwongozo wa kile unachoweza kukitarajia.

Usaili wa kazi, pamoja na mambo mengine, unapima uwezo wa mtafuta kazi kujieleza kwa ufasaha.

Wasaili wazuri, watakuuliza maswali magumu ili kuona unavyoweza kufikiri kwa haraka, kuchagua maneno kwa usahihi na hata kudhibiti hisia zako pale unapokasirishwa.

Usipoweza kujibu maswali unayoulizwa kwa umakini, unarahisisha kazi ya maofisa waajiri kufanya uamuzi wa kukuondoa kwenye ushindani.

Hapa ninakupa mfano wa maswali magumu yatakayokusaidia kujiandaa vyema na usaili.

Chukua tahadhari. Majibu haya si msahafu bali mifano tu ya kukupa mwongozo wa kile unachoweza kukitarajia.

Tuambie wewe ni nani?

Swali hili linakupa fursa ya kujieleza kwa uhuru. Mara nyingi litaulizwa mwanzo kabisa kama namna ya kuanza mazungumzo na wewe.

Wasailiwa wengi hulichukulia kirahisi kwa sababu hukimbilia kurudia yale yale waliyoyaandika kwenye barua ya maombi ya kazi na wasifu wa kazi matokeo yake wanaonekana hawana jipya mapema.

Unapoulizwa swali kama hili, kwanza kumbuka wanaouliza tayari wamesoma barua yako ya kuomba kazi na viambatanisho vyake. Wanajua umezaliwa lini, unaishi wapi na umesoma wapi. Unaporudia mambo wanayoyajua tayari unaonekana sio mbunifu.

Tumia swali hili kama fursa ya kujimbapanua eneo lako la utaalamu ni lipi, una ujuzi gani unaokuuza sokoni na umewahi kufanya vitu gani vinavyokubeba.

Usirudie yale uliyoyaandika kwenye wasifu wa kazi na barua ya maombi, ingawa unaweza kufanya marejeo ya hapa na pale.

Una udhaifu gani mkubwa?

Swali la namna hii linalenga kukuchokoza kupima uwezo wako wa kujibu maswali magumu. Jibu swali hili kwa hekima ukichagua sifa unazoziita ni ‘udhaifu’ lakini zikitazamwa kwa kina zinakubeba.

Unaweza kujibu, kwa mfano, ‘Udhaifu wangu mkubwa ni kufanya kazi kwa muda mrefu na wakati mwingine nasahau maisha mengine ya nje ya kazi.’ Hakuna mtu asiyependa kufanya kazi na mtu mwenye ‘udhaifu’ huu.

“Nina tabia ya kutaka kitu kifanyike kwa usahihi na umakini mkubwa kiasi kwamba saa nyingine naweza kujisikia hatia ninapofanya kazi na mtu anayetaka kulipua.” Kwa hiyo unaweza kuona, huo unaouita ‘udhaifu wako’ kimsingi ndiyo kile kile anachokitafuta mwajiri.

Kumbuka hakuna mtu anayetaka kuajiri mtu dhaifu hata kama ni kweli binadamu tuna upungufu wetu.

Usiingie kwenye mtego wa kusema ukweli usio na manufaa. Kuorodhesha udhaifu wako hata kama ndiyo ukweli wenyewe ni kukosa busara.

Kwa nini unaacha kazi huko uliko?

Huu ni mtego. Msaili anapouliza swali kama hili anataka kujua vile unavyomzungumzia mwajiri wako aliyepita. Usijibu swali hili kwa papara. Inawezekana ni kweli mwajiri wako wa sasa au aliyepita hakukulipa kile unachostahili. Usiwe mwepesi kuingia kwenye mtego wa kuonyesha ulivyoweka mbele masilahi. Inawezekana sababu halisi ni migogoro, kunyimwa haki zako za msingi na kero nyingine.

Kumbuka kuwa usaili wa kazi siyo mahali sahihi pa kuonyesha uwezo wako wa kuanika udhaifu wa wengine.

Jitahidi kuwa mtu chanya unayeweza kuona chema hata katika ubaya.

Jibu swali hili kwa kuonyesha kuwa unaacha kazi kwa sababu unafikiri bado kazi hiyo haijakupa fursa za kutumia vipaji vyako ipasavyo.

Jibu kama hili linamfanya msaili aamini unatafuta kazi inayokuwezesha kutumika zaidi.

Kwa nini tukuajiri?

Hapa muuliza swali anataka kuona unaleta thamani gani kwenye kampuni na upekee wako unaokutofautisha na washindani wengine. Hii, hata hivyo, siyo fursa ya kuwaponda washindani wako wala kuonyesha matamanio ya masilahi makubwa.

Jikite kumshawishi msaili aone kile ulichonacho kinachoweza kumletea tija kwenye huduma au biashara anayofanya.

Katika kutoa majibu yako, onyesha uelewa mpana wa shughuli za kampuni au taasisi unayoomba kufanya nayo kazi. Onyesha unafahamu kwa kina malengo yao na changamoto za kiutendaji wanazokabiliana nazo katika kufikia malengo hayo.

Ukishafanya hivyo, jielekeze kueleza unakuja na ufumbuzi gani ikiwa utapewa nafasi.

Tukulipe kiasi gani?

Swali hili ni gumu kidogo. Ingawa ni kweli unatafuta kazi itakayokulipa vizuri haipendezi kuonekana wewe ni mtu unayefuata mshahara. Mwajiri makini angependa kufanya kazi na mtu mwenye ari ya kazi isiyotegemea sana masilahi. Kusema hivyo, hata hivyo, haimaanishi akulipe usichostahili.

Jitahidi kujizuia kuzungumzia masuala yanayohusu mshahara wakati kazi yenyewe bado huna uhakika nayo. Kadri inavyowezekana, onyesha kuwa unaelewa kampuni au taasisi makini zina kiwango vya mshahara vinavyofahamika na kwamba uko tayari kulipwa kulingana na viwango vilivyopo.

Ikiwa unalazimika kueleza matarajio yako waziwazi, hakikisha umefanya utafiti wako vya kutosha. Taja kiwango cha mshahara kisicho mbali sana na viwango wanavyolipwa wenzako.

Kama unaamini unastahili zaidi, mazungumzo yasubiri utakapopewa barua rasmi ya ajira.

Christian Bwaya ni Mhadhiri wa Saikolojia, Chuo Kikuu cha Kikatoliki Mwenge (MWECAU). Mawasiliano 0754870815, twitter: @bwaya