Gama afariki dunia akipatiwa matibabu Peramiho

Muktasari:

Kabla ya kuwa mbunge Gama alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro.

Dar es Salaam. Mbunge wa Songea Mjini (CCM), Leonidas Gama amefariki dunia katika Hospitali ya Peramiho.

Akizungumza na Mwananchi leo Ijumaa Novemba 24,2017 mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Ruvuma, Oddo Mwisho amethibitisha msiba huo.

“Nimepata taarifa jana usiku (Alhamisi Novemba 23,2017) kuwa Gama amefariki kwa kuugua shinikizo la damu,’’ amesema.

Mwisho amesema, “Tunawasiliana na familia ili kujua utaratibu wa mazishi. CCM tunasikitika kwa msiba huu, msiba ni wetu sote.”

Kabla ya kuwa mbunge katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, Gama alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro.

Pia, amewahi kuwa Mkuu wa Wilaya ya Ilala mkoani Dar es Salaam.