Mzee wa miaka 104 aliyeomba kufa, kuchomwa sindano ya sumu

Muktasari:

Madaktari watampatia sindano yenye dawa ya kukatisha uhai wake ili ajichome mwenyewe

David Goodall, mwanasayansi aliyeomba kukatisha uhai wake, kesho atahitimisha safari yake duniani baada ya madaktari kuchomeka sindano ya sumu katika mshipa.

Mzee huyo wa miaka 104, atakaribisha kifo kwa usaidizi wa madaktari wanne Sheena McKenzie, Melissa Bell, Saskya Vandoorne na Ben Westcott nchini Uswisi.

Akihojiwa na Kituo cha CNN, Goodall amesema maisha yake hayana thamani tena ndio maana ameamua kuomba kujiua akiamini hadithi yake itakuwa mfano na kuhamasisha uamuzi kama huo kwa wengine waliochoka kuishi.

Goodall amelazimika kusafiri kutoka Australia mpaka Basel, Uswisi kukifuata kifo baada ya sheria za kwao kutomruhusu kufanya hivyo.

Babu huyo mwenye wajukuu 12 na mwanaharakati wa kundi la Exit International linalopigania haki ya kujiua, amesema maisha yake yalisimama miaka 10 iliyopita baada ya kupoteza uoni na uwezo wa kutembea.

"Natamani ningekuwa na uwezo wa kutembea mashambani na kuona vitu vinavyonizunguka,” amesema Goodall baba wa watoto wanne kutoka kwa wake watatu aliowahi kuwa nao.

Amesema anatamani kifo kingemchukua alipotimiza miaka 94 kwani wakati huo ndio aliponyang’anywa leseni yake ya udereva baada ya kupoteza uoni.

"Katika umri huu naamka asubuhi, nakunywa chai. Nasubiri mchana nile halafu sina cha kufanya tena. Maisha ya aina hii ya kazi gani? Anahoji Goodall.

Nchini Australia kifo cha hiyari hakijaruhusiwa ingawa jimbo la Victoria linapanga kuruhusu kuanzia mwakani.

Goodall amesema amepatwa na hasira kuona analazimika kusafiri mpaka Uswisi kuipata haki ya kujiua, lakini anaamini tukio lake litaleta mabadiliko kwa wengine.

"Naisubiri saa yangu ya kufa kwa hamu kubwa, nina furaha pia kupata nafasi ya kuhojiwa kwa kuwa stori yangu inakwenda kwenye kumbukumbu za dunia. Ushauri wangu ni nchi zote duniani kuiga mfano wa Uswisi,” amesema.

Kesho, madaktari wataweka sindano iliyojazwa dawa ya sodium pentobarbital katika mshipa wake na kumuacha aisukume mwenyewe kwenda mwilini mwake.

Goodall alizaliwa katika Jiji la London Aprili 1914, ikiwa ni mwezi mmoja kabla ya kuanza kwa vita ya kwanza ya dunia.