TRA yakataa kuuza bidhaa mojamoja ndani ya makontena ya Makonda

Muktasari:

  • Makontena hayo yaliyoletwa Februari, hayakulipiwa kodi inayofikia Sh1.2 bilioni hivyo yanapigwa mnada.

Dar es Salaam. Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imesema haitauza bidhaa mojamoja kutoka kwenye makontena 20 ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda hata kama hayauziki.

Makontena hayo yaliyoletwa Februari, hayakulipiwa kodi inayofikia Sh1.2 bilioni hivyo yanapigwa mnada.

Hata hivyo, licha mnada huo kuitishwa mara mbili yameshindwa kuuzika kwa kuwa wateja wameshindwa kufikia bei.

Akizungumza na Mwananchi kwa simu jana, Mkurugenzi wa Elimu na Huduma kwa Mlipakodi wa TRA, Richard Kayombo alisema haiwezekani kuuza bidhaa mojamoja kwenye makontena hayo kwa sababu zipo nyingi.

“Hatuwezi kuuza item (kitu kimoja) mojamoja kwa sababu ni nyingi mno, tutakesha. Tunauza kwa ‘lot’ ndiyo maana huwa tunatangaza vilivyomo ndani. Sio makontena ya Makonda tu, kuna ‘lot’ nyingi sana na kila jumamosi tuna mnada,” alisema Kayombo.

Alipoulizwa hatua watakayochukua endapo makontena hayo hayatauzika kwa muda mrefu, Kayombo alisema: “Hayo ni mambo ya utawala, tutajua la kufanya kama hayauziki.”

Kuhusu bei ya makontena hayo, Kayombo alisema ni siri yao.

“Bei hatutangazi, hiyo ni siri yetu. Hata kanisani unaponadi kitu hutaji bei. Mnada ni bei ifike au izidi,” alisema.

Awali, Mkurugenzi wa Yono Auction Mart, Scholastica Kevela alisema utaratibu wa mnada unatolewa na TRA.

“Utaratibu wa mnada unatolewa na TRA, halafu hizo items ni nyingi sana kiasi kwamba itachukua muda mrefu kupiga hesabu. Je, kodi itafika” alisema.

Alisema wateja walipata nafasi kukagua bidhaa kwenye makontena yote 20 na kujiridhisha.

“Mteja analalamika kuwa kontena limepunguzwa mzigo, kwani alikuwapo wakati wa kupakia? Wateja walipata nafasi ya kukagua tangu Alhamisi na Ijumaa iliyopita,” alisema.