Takwimu: Wanafunzi 78 wapoteza maisha kwa ajali za barabarani

Wanafunzi jijini Dar es Salaam wakivuka barabara. PIcha ya Mtandaoni

Muktasari:

Jeshi la polisi nchini limesema wanafunzi 78 nchini wamepoteza maisha kutokana na ajali za barabara huku 181 wakijeruhiwa katika kipindi cha mwaka 2015.

Dar Es Salam. Jeshi la polisi nchini limesema wanafunzi 78 nchini wamepoteza maisha kutokana na ajali za barabara huku 181 wakijeruhiwa katika kipindi cha mwaka 2015.

Hayo aliyasema leo na Mnadhimu wa Kikosi cha Usalama barabarani kutoka Makao Makuu,  Fortunatus Muslim wakati wa  utoaji  zawadi  kwa washindi wa shindano la uchoraji alama za usalama barabarani.

Muslim alisema kati ya wanafunzi 78 waliofariki, wavulana walikuwa 40 na wasichana 38, huku majeruhi wakiwa 181 ambapo kati ya hao wavulana walikuwa 81 na wa kike 81.

"Maeneo hatarishi ambayo yanaongoza kwa  kusababisha ajali za barabarani katika Jiji la  Dar  Es Salaam ni Lumumba, Mnazi mmoja, Mikumi, Mtambani, Boko, Bunju na Kongowe." Alisema Muslim.

Mashindano hayo ambayo yaliandaliwa na kampuni ya Puma Energy yalilenga kutoa elimu kwa wanafunzi wa shule za msingi juu  ya utumiaji wa alama  za usalama barabarani.

"Jeshi  la Polisi kupitia kikosi cha usalama barabarani limeendelea kutoa elimu kwa wanafunzi, madereva na Jamii kwa ujumla juu  ya matumizi sahihi ya barabarani" aliongeza Muslim

Alisema wanafunzi walioshinda shindano la uchoraji wa alama za usalama barabarani ni Shaibu Abdalah kutoka shule ya msingi Gongo la mboto,  Abdallah Hussein kutoka Osterybay  na Christian Mathias kutoka Gongo la mboto.

Awali, Meneja  wa kampuni ya Puma Enegy, Philippe Corsaletti alisema lengo la  mashindano hayo ni kutoa elimu kwa wanafunzi kuhusiana na matumizi sahihi ya barabarani.