Wafurika kumwangalia Zari Mlimani City

Muktasari:

  • Zari alikuwa katika duka la Danude lililoko Mlimani City kwaajili ya uzinduzi wa duka hilo

Dar es Salaam. Mpenzi wa mwanamuziki Diamond Platnumz, Zari mchana wa leo Jumamosi alisimamisha shughuli katika maduka yaliyopo Mlimani City alipokwenda kuzindua duka jipya la samani, Danube.

Wakazi wa jiji la Dar es Salaam waliofika kufanya manunuzi katika maduka hayo walijazana nje ya duka jipya la Danube wakitaka kumuona Zari huku wakiimba wifi... wifi.

Purukushani zilitawala nje ya duka hilo wakati kila mmoja akijaribu kumsukuma mwenzake ili aweze kumuona Zari aliyekuwa ameketi katika makochi akizungumza na wafanyakazi.

Watu walivutiwa kumuona mwanamke huyo kutokana na hivi karibuni kupamba vichwa vya habari baada ya Diamond kukiri kuzaa na mwanamitindo Hamisa Mobetto.

Ujio wa Zari nchini amekuwa na mvuto kwa kuwa mashabiki wamekuwa wakilinganisha matukio katika maisha ya Diamond, Zari na Hamisa.

Siku moja kabla ya Zari kutoa tangazo kuwa angeshiriki uzinduzi wa duka jipya la Danube, mwanamitindo Hamisa aliweka tangazo la duka hilo ambalo liliwahi kufanywa na Diamond na Zari mapema mwaka huu.

Katika tangazo hilo Zari alisikika akimpiga kijembe mwanamke aliyeacha hereni nyumbani kwa Diamond, Madale jijini Dar es Salaam akimtaka aende akachue.

Katika posti yake kwenye mtandao wa Instagram, Hamisa aliandika: “It’s about time nifuate hereni zangu, I hope they are still there.” Akimaanisha umefika wakati nifuate hereni zangu, nadhani zitakuwepo.