Pasta Uganda kortini kwa kusema corona haipo Afrika

Muktasari:

Hadi sasa Uganda imeripoti kuwa na watu 33 walio na maambukizi ya virusi vya corona na imezuia usafiri wa umma kuepuka misongamano.

Mamlaka nchini Uganda zimemfungulia mashtaka na kumfunga muhibiri wa injili ambaye anatuhumiwa kukana uwepo wa virusi vipya vya corona barani Afrika, polisi wamesema leo.
Muhubiri huyo maarufu, Augustine Yiga, anatuhumiwa na waendesha mashtaka kuwa aliwaambia waumini wa kanisa la Ufufuo wa Kikristo Ijumaa na maneno yake kutangazwa na vituovya televisheni kuwa "nchini Uganda na barani Afrika hakuna virusi vya corona".
"Pasta Yiga wa Kanisa la Ufufuo wa Kikristo ameshtakiwa na yuko mahaburu kwa kufanya vitendo ambavyo vinaweza kusambaza Covid-19," Patrick Onyango, msemaji wa polisi, alisema.
"Kudai kwamba Covid-19 haipo Afrika wala Uganda kunafanya juhudi za serikali kupambana na ugonjwa huo wa dunia kuwa hazina maana na kunauweka umma katika hatari kubwa zaidi ya kutozingatia miongozi ya kudhibiti na kujikinga," alisema.
Lakini mwanasheria wa pasta huyo, Wilberforce Kayiwa, alisema Yiga alikana shtaka la kuendeleza maambukizi ya virusi hivyo.
Kiongozi huyo wa kidini anakabiliwa na kifungo cha hadi miaka saba jela.
Yiga, ambaye anaendesha kanisa na kituo cha televisheni, ana wafuasi wengi na anajulikana kwa kutoa kauli zenye utata na kudai ana nguv u za kinabii.
Hadi sasa, Uganda imeripoti watu 33 wenye maambukizi ya virusi vya corona.
Rais wa Uganda, Yoweri Museveni amewataka wananchi kubakia majumbani lakini hajatoa amri ya kutotoka nyumbani.
Shule, maeneo ya burudani na ya kuabudia na baadhi ya masoko ya bidhaa za kilimo, yamefungwa kwa muda wa mwezi mmoja na watu wamepigwa marufuku kusafiri kwa kutumia usafiri wa umma na kuwa zaidi ya watu watatu ndani ya gari, au zaidi ya mmoja katika pikipiki.
Wiki iliyopita, watu sita raia wa China na Waganda wawili walishtakiwa kwa kufanya kitendo ambacho kinaweza kusababisha kusambaa kwa maambukizi ya virusi hivyo baada ya kutoroka hotelini walikokuwa wamewekwa chini ya karantini.
Watu wawili kati ya raia hao wa China waligundulika kuwa na maambukizi.