Rais Malawi ahaha kujinasua

Muktasari:

Rais wa Malawi, Peter Mutharika amesema kuwa atakata rufaa kupinga uamuzi wa mahakama uliofuta matokeo ya uchaguzi mkuu.

Lilongwe, Malawi. Rais wa Malawi, Peter Mutharika ametangaza kusudio la kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa Mahakama ya kikatiba uliomvua madaraka.

Jumatatu iliyopita mahakama hiyo ya Malawi ilitangaza kutengua matoeo ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2019 uliompa ushindi Rais Mutharika. Hata hivyo vyama vya upinzani nchini huo vilifungua kesi kupinga ushindi huo uliofanyika mwezi Mei.

Majaji watano wa mahakama hiyo walisema uchaguzi huo ulikuwa na kasoro kadhaa ikiwamo matumizi ya wino bandia hivyo ushindi wa Mutharika haukuwa halali.

Msemaji wa Rais Mutharika, Mgeme Kalilani, alisema jana kuwa hukumu hiyo ilikuwa na upotoshaji wa haki na shambulio dhidi ya misingi ya demokrasia nchini Malawi.

Hata hivyo, Mgeme hakuweka baya rufaa hiyo itawasilishwa lini. Kwa sasa kiongozi huyo anao muda wa wiki sita kisheria kuwasilisha rufaa hiyo.

Akizungumzia hukumu hiyo, kiongozi wa chama kikuu cha upinzani nchini humo, Lazarus Chakwera alisema ni ushindi kwa demokrasia na Afrika.

Aliongeza kuwa hukumu hiyo ni ya historia katika bara la Afrika.