Uchaguzi wa serikali za mitaa, Majaliwa atoa maagizo kwa wabunge, Ma RC na DC

Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa

Muktasari:

  • Mkutano wa 16 wa Bunge ulioanza Septemba 3, 2019 jijini Dodoma umehitimishwa leo Ijumaa Septemba 13, 2019 kwa Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa kutoa wito kwa wabunge, wakuu wa mikoa na wilaya kuhusu uchaguzi wa serikali za mitaa utakaofanyika Novemba 24, 2019.

Dodoma. Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amewaagiza wabunge, wakuu wilaya (DC) na mikoa (RC) kuwahamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi katika uchaguzi wa serikali za mitaa Novemba 24,2019.

Majaliwa  ametoa kauli hiyo leo Ijumaa  Septemba 13, 2019 wakati akitoa hotuba ya kuahirisha shughuli za mkutano wa 16 wa Bunge la Tanzania akusema ni haki ya kila mwananchi kutumia nafasi hiyo kupiga kura.

Kiongozi huyo ameviomba vyombo vya ulinzi na usalama kusaidia uchaguzi huo kuwa wenye uhuru na haki huku akiwahamasisha wenye sifa kugombea nafasi mbalimbali katika serikali za mitaa.

"Nawaomba wote wenye sifa wajitokeze kugombea nafasi hizo ili watumie nafasi hiyo kuchaguliwa na kuwa viongozi wa maeneo yao," amesema Majaliwa.

Majaliwa pia amewahimiza wananchi kuhifadhi vyakula katika msimu huu akisema  maandalizi ya msimu wa kilimo kwa maeneo mengine umeanza.