Samatta atokea mlango wa uani

Dar es Salaam. Wakati mamia ya wakazi wa Kichangani wikisubiri kumuona nahodha wa Taifa Stars, Mbwana Samatta na kumpongeza kwa kubeba jiko, staa huyo amelazimika kutolewa kupitia mlango wa uani baada ya kumaliza kufungishwa ndoa.

Samatta amefunga ndoa usiku huu na mchumba wake Neima Mgange akisindikizwa na baba yake mzazi Mzee Ally Samatta na ndugu wengine.

Pia winga wa JS Saoura Thomas Ulimwengu na Himid Mao walikuwa miongoni mwa mashuhuda.

Awali baada ya wakazi wa mtaa huo kubaini kuwa Samatta ndiye anayemuoa Neima, walikusanyika nyumbani hapo wakisubiri kumuona.

Hata hivyo, wapambe waliomsindikiza Samatta wakaona hakuna namna zaidi ya kumtoa kupitia mlango wa uani akipewa kampani kubwa na Ulimwengu.

Lakini, mbinu hiyo ikashtukiwa kwa haraka na kundi hilo wakiwemo vijana na akina mama wa mtaa huo na maeneo ya jirani, wakaenda kulizingira gari lililombeba huku wakimuomba atoke japo kidogo tu wamuone.