ACT yatafakari kujiunga Serikali ya Umoja ya Kitaifa Zanzibar

Mwenyekiti wa ACT Wazalendo, Maalim Seif Sharif Hamad

Muktasari:

Chama cha ACT-Wazalendo kimesema kinajipa muda zaidi wa kutafakari iwapo itapendekeza jina la makamu wa kwanza wa rais wa Zanzibar pamoja na kushiriki katika Serikali ya Umoja ya Kitaifa (SUK).

Dar es Salaam. Chama cha ACT-Wazalendo kimesema kinajipa muda zaidi wa kutafakari iwapo itapendekeza jina la makamu wa kwanza wa rais wa Zanzibar pamoja na kushiriki katika Serikali ya Umoja ya Kitaifa (SUK).

Kauli hiyo ilitolewa jana na Mwenyekiti wa ACT Wazalendo, Maalim Seif Sharif Hamad wakati akizungumza na gazeti hili lililotaka kujua msimamo wa chama hicho kuhusu ushiriki wake katika SUK, kutokana na msimamo wake wa awali kutotambua Uchaguzi Mkuu uliopita na matokeo yake.

Kwa mujibu wa Ibara ya 39 ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 2010, Rais wa Zanzibar atamteua Makamu wa Kwanza wa Rais mwenye sifa za kuwa mjumbe wa Baraza la Wawakilishi na atateuliwa na Rais baada ya kushauriana na chama kilichotokea nafasi ya pili katika matokeo ya kura ya Uchaguzi wa Rais.

Hata hivyo, chama kilichotokea nafasi ya pili katika uchaguzi kinatakiwa kiwe kimepata si chini ya asilimia 10 ya kura zote.

Katika matokeo ya urais Zanzibar yaliyotangazwa Oktoba 29, mwaka huu Maalim Seif aliyegombea urais kupitia ACT alipata asilimia 19.87.

Kwa mujibu wa Katiba hiyo ya Zanzibar, pamoja na uteuzi huo na Rais atafanya mashauriano kuhusu uteuzi wa mawaziri kutoka upinzani.

Kulingana na katiba hiyo iliyotokana na maridhiano ya mwaka 2010 yaliyofanyika baina ya Rais wa sita Amani Abeid Karume na Maalim Seif, makamu wa kwanza wa Rais atakuwa ni mshauri mkuu wa Rais katika kutekeleza kazi zake na atafanya kazi zote atakazopangiwa na Rais.

Ndani ya siku saba zinazotajwa na Katiba, Dk Mwinyi amemteua Hemed Suleiman Abdulla kuwa mjumbe wa Baraza la Wawakilishi na kisha Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.

Baada ya muda huo kupita na kimya kutawala kuhusu nafasi ya makamu wa kwanza wa Rais, Mwananchi lilimtafuta mwenyekiti huyo wa ambaye alisema bado kuna muda kwa kuwa Katiba ya Zanzibar inatoa siku 90 kwa chama kitakachotoa makamu wa kwanza wa rais kupeleka jina ikiwa hakikuweza kufanya hivyo katika siku saba za mwanzo.

“Kamati kuu (ya ACT Wazalendo) iliamua tusikimbilie katika siku saba kwa sababu kuna mambo yanayohitaji tafakuri ya kina. Pia katika jambo kubwa kama hili na mazingira ya huu unaoitwa uchaguzi ni vizuri kuwashirikisha wanachama wenzetu katika kutoa ushauri wao kwa kuwa ndio waathirika,” alisema Maalim Seif.

Alipoulizwa watawashirikishaje wanachama hao, Maalim Seif ambaye aliwahi kuwa makamu wa kwanza wa Rais Zanzibar alisema “kuwashirikisha wanachama wetu sio jambo geni. Tunafanya vikao vya ndani na wanachama katika maeneo mbalimbali ya Unguja na Pemba na kuwaomba watoe maoni yao kwa uhuru.”

Maalim Seif ambaye pia aliwahi kuwa Waziri Kiongozi wa Zanzibar alisisitiza kuwa ACT-Wazalendo imeamua kujipa muda wa kutosha katika kufanya uamuzi wa suala hilo huku akisema kuhusu ushirikishwaji wa wananchi chama kinajipanga pia.

Kwa nyakati tofauti Rais wa awamu ya nane wa Zanzibar, Dk Mwinyi aliyepata kura 380,402 sawa na asilimia 76.27, amesema ataendeleza maridhiano yaliyopo kikatiba pamoja na kudumisha amani iliyopo kwa kushirikiana na wapinzani kwa kuwa ni nyenzo muhimu katika kukuza demokrasia nchini.