Alichokisema Ngeleja kuhusu kumuomba msamaha Magufuli

Mbunge wa Sengerema (CCM), William Ngeleja

Muktasari:

Mbunge wa Sengerema (CCM), William Ngeleja leo Alhamisi Septemba 12, 2019 amezungumza kwa mara ya kwanza tangu Rais wa Tanzania, John Magufuli alipotangaza kumsamehe pamoja na mwenzake, January Makamba (Bumbuli).

Dodoma. Mbunge wa Sengerema (CCM), William Ngeleja leo Alhamisi Septemba 12, 2019 amezungumza kwa mara ya kwanza tangu Rais wa Tanzania, John Magufuli alipotangaza kumsamehe pamoja na mwenzake, January Makamba (Bumbuli).

Ngeleja amezungumza bungeni mjini Dodoma katika mjadala wa muswada wa Sheria Mbalimbali namba 6 wa mwaka 2019, akimshukuru Spika wa Bunge, Job Ndugai kuwapongeza wabunge waliomuomba msamaha Rais Magufuli.

Ngeleja na Makamba walikuwa wabunge wa kwanza kumuomba radhi Magufuli kufuatia kuhusishwa na  sauti zilizosambaa mitandaoni zikizungumzia barua ya makatibu wa zamani wa CCM na pia hali ya chama kudhoofika na kumkejeli kiongozi mkuu huyo wa nchi.

Juzi mbunge wa Mtama, Nape       Nnauye naye aliomba msamaha na kuwa mtu wa tatu kati ya wanachama sita wa chama hicho tawala waliohusishwa na sauti hizo.

Akizungumza bungeni Ngeleja amesema, “Kibinadamu wote tunajua msamaha siku zote unaleta faraja. Mimi mwenyewe lakini kwa niaba ya wananchi wa Sengerema nitumie nafasi hii kuelezea faraja niliyonayo kwa kupata huo msamaha. Pia, nakushukuru (Ndugai) kwa namna ambavyo umeliweka.”

Mapema leo Ndugai aliwapongeza wabunge hao kwa kuomba msamaha, ““Nawapongeza wabunge wangu watatu kwa jambo muhimu la kuomba radhi kwa Rais kwa yaliyotokea. Kwa binadamu wa kawaida kuomba radhi si jambo la kawaida na wengi wameshindwa kufanya hivyo.”