VIDEO: Bilioni 1 ilivyotumika kukodi makazi ya balozi tatu

Muktasari:

  • CAG Kichere amesema kiasi hicho cha fedha kingeweza kuepukika kama Balozi hizo zingekarabati nyumba zao za makazi

Dar es Salaam. Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere amesema katika ukaguzi wake unaoishia Juni 30, 2019 amebaini Balozi za Tanzania nchini Brazil, Nigeria na Stockholm/Sweden zimetumia Sh1.02 bilioni kukodi nyumba za makazi.


Kichere ameyasema hayo leo Machi 26 jijini Dodoma wakati akiwasilisha ripoti yake kwa Rais John Magufuli ya ukaguzi wa mwaka 2018/19.
Kichere amesema kiasi hicho cha fedha kingeweza kuepukika kama balozi hizo zingekarabati nyumba zao za makazi.


Pia, Kichere amesema katika ukaguzi wake amebaini kwamba balozi 14 za Tanzania zina majengo ambayo yametelekezwa, hivyo ameshauri majengo hayo kukarabatiwa ili kuokoa fedha ambazo zinatumika kukodi nyumba.


Amezitaja baadhi ya balozi hizo kuwa ni pamoja na Canada, Burundi, Kenya, Sweden na Algeria.