Dk Bashiru ataja kitakachoipa ushindi CCM uchaguzi 2020

Muktasari:

  • Katibu mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally amesema utekelezaji wa mambo mbalimbali unaofanywa na Serikali inayoundwa na chama hicho tawala ndio utatumiwa kuomba kura katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.

Kigoma. Katibu mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally amesema utekelezaji wa mambo mbalimbali unaofanywa na Serikali inayoundwa na chama hicho tawala ndio utatumiwa kuomba kura katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.

Dk Bashiru ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Januari 17, 2020 katika kata ya Kazuramimba wilayani Kigoma wakati akizungumza na viongozi wa chama hicho pamoja na jumuiya zake.

Dk Bashiru amesema CCM haitegemei kupata ushindi siku ya uchaguzi, akibainisha kuwa kura haziji kama mvua, hupigwa na mtu aliyefikiria kwa miaka mitano si siku moja.

"Kama wao wanasubiri kura za kunyesha kama mvua au wanadhani wakipita kusema uongo na kujinadi na bendera wakati wa kampeni watapata kura wanakosea,” amesema Dk Bashiru

Amesema CCM walianza kutafuta kura za wananchi tangu chama hicho kilipoibuka na ushindi katika uchaguzi wa mwaka 2015, kuunda Serikali.

Ametaja baadhi ya utekelezaji wa mambo hayo kuwa ni ujenzi wa vituo vya afya, reli ya kisasa, shule, miradi ya maji, barabara, umeme.