Dk Bashiru azifariji familia Pemba

Muktasari:

Katibu Mkuu wa CCM Dk Bashiru amezitembelea familia zilizokumbwa na kadhia ya mafuriko na kuzitaka kuwa na subira akifahamu zilipoteza mali.

Pemba. Katibu Mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally amezitaka familizia zilizokumbwa na mafuriko katika shehia ya Kiuyu Minungwini wilaya ya Micheweni mkoa wa Kaskazini Pemba kuwa na subira katika kipindi hichi kigumu kwao.

Dk Bashiru ameyasema hayo leo Desemba 2 wakati akiwa katika ziara yake ya siku ya kwanza kisiwani hapa.

Amesema anafahamu kuwa familia hizo zilizokumbwa na kadhia hiyo zilipoteza mali nyingi lakini hawana budi kumshukuru Mungu wakitambua kuwa kila jambo ni mipango yake.

Katika hatua nyingine Dk Bashiru alizifariji familia hizo kwa kuzipatika vifaa mbali mbali ambavyo vitawafanya waweze kujikimu katika kipindi hichi cha mpito kwa familia hizo.

Dk Bashiru pia ameshiriki katika ujenzi wa tawi la chama hicho lililopo Kiuyu Minungwini wilaya ya Micheweni mkoa wa Kaskazini Pemba na kuchangia shilingi milioni mbili kama sehemu ya kuendeleza ujenzi huo.