James Mapalala afariki dunia

Muktasari:

  • Mwanasiasa aliyejitosa kudai mfumo wa vyama vingi urejeshwe nchini Tanzania, James Mapalala amefariki dunia leo Jumatano Oktoba 23, 2019 katika Hospitali ya Kairuki jijini Dar es Salaam.

Dar es Salaam. Mwanasiasa mkongwe nchini Tanzania, James Mapalala amefariki dunia katika hospitali ya Kairuki alikokuwa akipatiwa matibabu.

Akizungumza na Mwananchi leo Jumatano Oktoba 23, 2019 mtoto wa mwanasiasa huyo, Bernard James amesema baba yake amefariki dunia leo saa  4:30 asubuhi.

“Alikuwa hospitali tangu wiki mbili zilizopita baada ya kusumbuliwa na maradhi ya kupumua,” amesema James.

Amesema familia imekusanyika nyumbani kwao Kinondoni kupanga ratiba ya mazishi.

Mapalala aliyezaliwa Februari Mosi, 1936 ameacha mke na watoto kadhaa.

Alikuwa miongoni mwa wanasiasa wa kwanza waliojitosa kudai mfumo wa vyama vingi urejeshwe nchini Tanzania.

Kufuatia madai hayo, Mapalala alifungwa miaka miwili mkoani  Lindi kuanzia mwaka 1986 hadi 1989 na baada ya kutoka aliwekwa kizuizini kwa kipindi cha mwaka mmoja katika kisiwa cha Mafia baada ya  kuanzishwa chama cha siasa wakati sheria ilikuwa hairuhusu.

Alianzisha Chama cha Wananchi (CCW) mwaka 1991 na baadaye kiliungana na chama cha Zanzibar – Kamahuru na mwaka 1993 kuzaliwa Chama cha Wananchi (CUF).