Jinsi mgonjwa wa corona alivyoingia Tanzania hadi akagundulika

Muktasari:

Leo Jumatatu Machi 16, 2020 kupitia kwa Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amethibitisha kuwapo mgonjwa wa kwanza mwenye virusi vya corona.

Dar es Salaam. Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema kuwa tarehe 15 Machi 2020, katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) walipokea msafiri raia wa Tanzania mwanamke mwenye umri wa miaka 46, ambaye aliwasili na ndege ya Rwanda akitokea nchini Ubelgiji.
Waziri Ummy amesema kuwa msafiri huyo aliondoka tarehe 3 Machi 2020, ambapo kati ya tarehe 5-13 Machi alitembelea nchi za Sweden na Denmark na kurudi tena Ubelgiji na kurejea nchini tarehe 15 Machi saa 10 jioni.
Ameeleza kuwa msafiri huyo alipita uwanja wa KIA na kufanyiwa ukaguzi na kuonekana kutokuwa na homa lakini  baadae alianza kujisikia vibaya akiwa hotelini na kwenda hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Mt. Meru.
Mara baada ya kufika hospitalini alifanyiwa vipimo na kisha  sampuli ilichukuliwa  na kupelekwa maabara ya Taifa ya afya iliyopo Dar es Salaam kwa ajili ya uchunguzi.
Baada ya vipimo vya maabara kufanyika vimethibitisha kuwa mtu huyo ana maambukizi ya ugonjwa wa corona (COVID-19), ambapo waziri Ummy amesema mgonjwa anaendelea vizuri na matibabu.
Waziri Ummy amewatoa hofu Watanzania kwa kusema Serikali imejiandaa vyema kukabiliana na ugonjwa huo huku akiwataka watu kuendelea kuchukua tahadhari zaidi.