Katibu mkuu CUF afariki dunia, kuzikwa leo

Muktasari:

Katibu Mkuu wa CUF, Khalifa Suleiman Khalifa amefariki dunia usiku wa kuamkia leo Jumanne Machi 31 2020 katika hospitali ya Aga Khan alikokuwa akipatiwa matibabu.

Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa CUF, Khalifa Suleiman Khalifa amefariki dunia usiku wa kuamkia leo Jumanne Machi 31 2020 katika hospitali ya Aga Khan alikokuwa akipatiwa matibabu.

Akizungunza na Mwananchi, mwanaye  Said Khalifa  amesema tangu Januari 2020 kwa nyakati tofauti baba yake aliugua na kulazwa katika hospitali hiyo.

"Karibu mara tatu mzee alilazwa Aga Khan akipatiwa matibabu na akipata ahueni tulikuwa tunarudi nyumbani kujisikilizia. Kwa sasa siwezi kuzungumza kwa kirefu nahisi nimechanganyikiwa naomba unitafute baadaye," amesema Said.

Machi 16, 2019 Khalifa akichaguliwa na baraza kuu la uongozi la CUF kuwa katibu mkuu wa pili wa chama hicho akichukua nafasi ya Maalim Seif Sharif Hamad ambaye alivuliwa uanachama.

 

Mwili wa Khalifa utazikwa leo katika makaburi ya Kisutu wilayani Ilala, Dar es Salaam.