Lukuvi amtumbua Mkuu wa idara ya ardhi Manispaa ya Iringa Tanzania

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Willium Lukuvi akizungumza na wananchi wa iringa katika ukumbi wa siasa na kilimo wakati akisikiliza kero za ardhi katika kampeni ya Funguka kwa Waziri.

Muktasari:

  • Kuna watendaji ambao hujisahau hawajui kama wapo katika ofisi za Serikali, wanatumia muda na ofisi za serikali kufanya kazi zao binafsi kwa kujiingizia vipato.

Iringa. Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi amemvua ukuu wa idara ya Mipango Miji ofisa ardhi wa manispaa ya Iringa, Willbard Mtongani baada ya kugundua anatumia ofisi ya serikali kuendesha kazi zake binafsi.

Lukuvi amemvua ukuu wa idara ya Mipango Miji ofisa huyo leo Desemba 2, 2019, wakati akisikiliza na kutatua kero za wananchi katika ukumbi wa Siasa ni Kilimo mjini Iringa.

Lukuvi amesema, wapo watendaji ambao wanajisahau hawajui kama wapo katika ofisi za Serikali, wanatumia muda na ofisi ya serikali kufanya kazi zao binafsi kwa kujiingizia kipato.

“Hapa Iringa wapo wananchi wanapata matatizo ya ardhi badala ya kusaidiwa na ofisi ya serikali ipate mapato, wanawapeleka kwenye ofisi zao binafsi, hivyo namvua ukuu wa idara ya ardhi Willbard Mtongani kama mfano kwa watendaji wote wanaounganisha ofisi ya serikali na ofisi zao binafsi ili na wengine wajifunze,” amesema.

Ameahidi kuendelea kumchunguza ofisa huyo ili kujua fedha alizovuna kwa utaratibu huo alioutaja kuwa ni kinyume na utaratibu.