Madini ya tini sasa rasmi Tanzania

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akitazama madini wakati alipotembelea banda la kampuni ya Kisangani Smith Group ya mkoani Njombe katika maonesho yaliyokwenda sambamba na Mkutano wa Kimataifa wa Uwekezaji Katika Sekta ya Madini Tanzania wa Mwaka 2020 ulioufungwa na Waziri Mkuu kwenye Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar es salaam, Februari 23, 2020. Kushoto ni Waziri wa Madini, Doto Biteko na watatu kushoto ni Spika wa Bunge, Job Ndugai.

Muktasari:

Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amezindua rasmi cheti halisi cha madini ya tini (bati) ambayo yanachimbwa kwa wingi wilayani Kyerwa mkoani Kagera.

Dar es Salaam. Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa leo Jumapili Februari 23, 2020 amezindua rasmi cheti halisi cha madini ya tini (bati) yanachimbwa kwa wingi Wilayani Kyerwa mkoani Kagera.

Majaliwa amezindua cheti hicho jijini Dar es Salaam wakati wa ufungaji wa mkutano wa uwekezaji kwenye sekta ya madini.

Mkutano huo ulioanza jana Jumamosi Februari 22, ulijumuisha nchi 11 za ukanda wa maziwa makuu, wamiliki wa kampuni za utafiti na uchimbaji madini kutoka ndani na nje ya nchi, wachimbaji wadogo, washirika wa maendeleo na mabalozi.

Akizungumza na wawekezaji hao, Majaliwa amepongeza uzinduzi huo ambao utaifanya Tanzania kuwa nchi ya kwanza kupata cheti hicho na itaanza kudhibiti na kufuata taratibu zote za kuchimba madini hayo.

“Nitoe wito kwa nchi wanachama kuhakikisha mikutano ya aina hii inaandaliwa katika nchi nyingine na iwe endelevu ili kutoa hamasa kwa wadau kutambua fursa zilizopo katika kila nchi ambayo ina madini,” amesema Majaliwa.

Amesema sekta ya madini Tanzania inazidi kuimarika na inaongeza mchango mkubwa kwenye pato la Taifa.

 Amesema katika ripoti ya hali ya uchumi ya mwaka 2019 katika kipindi cha nusu ya kwanza ya mwaka wa fedha 2019/20, mchango wa sekta ya madini ulikuwa kwa asilimia 13.7 ikiwa ya pili baada ya sekta ya ujenzi.

Kabla ya kufunga mkutano huo, Waziri wa madini, Doto Biteko alisema lengo kuu la mkutano huo ambao unafanyika kwa mara ya pili nchini ni kutoa fursa kwa wadau wa madini kutambua fursa za uwekezaji ambazo zipo nchini na kubadilishana ufahamu, uzoefu na teknolojia

“Kujenga uhusiano na ushirikiano wa kibiashara wa shughuli za uchimbaji na utafutaji. Pia kutoa fursa kwa taasisi kusikiliza na kupata maoni mbalimbali ya wadau kwa lengo la kuboresha,” amesema Biteko.

Amesema taarifa za kuwa wawekezaji wanakimbia nchini si za kweli kwa sababu wameshiriki vikao hivyo na kuna maombi mengi ya leseni yamewasilishwa kutoka ndani na nje ya nchi.

“Kwenye mchakato tunazo leseni kubwa mbili za uchimbaji madini ambazo mtaji wake ni kuanzia dola 100 milioni na moja ni ya kuendelea kuchimba dhahabu,” amesema Biteko.