Magufuli ampa agizo Makonda kuhusu miradi ya Coco Beach

Muktasari:

Rais Magufuli atoa maagizo wa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kuhusu miradi ya Coco Beach na Vingunguti, ataka ikamilike kwa wakati kwa kuwa fedha zimeshatolewa kwa ajili ya utekelezaji

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, John Magufuli amemwagiza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kuhakikisha miradi ya Coco Beach na machinjio Vingunguti yenye thamani Sh26.47 bilionii inakamilika kwa wakati.

Mradi wa Vingunguti una thamani ya Sh12.47bilioni ambao ukikamilika ng’ombe 1,000 na mbuzi 500 watakuwa wakichinjwa kila siku, wakati mradi wa uboreshaji wa ufukwe wa Coco Beach ukigharimu Sh14 bilioni.

Rais Magufuli ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Septemba 10, 2019 wakati akizundua kiwanda cha  kutengeneza mabomba cha Pipe Indrustries Ltd kilichopo Vingunguti wilayani Ilala jijini humo.

 Mkuu wa nchi  huyo amesema mradi Vingunguti bado haujengwa kuna mabishano wakati Serikali imeshatoa fedha Sh12.5bilioni. 

“Nataka mradi huo ukamilike, haiwezekani watu wanachinjia mbuzi chini nitakuja siku moja nivamie pale. Fedha zipo lakini miradi haikamiliki ndilo tatizo la Dar es Salaam. Kule Coco Beach tulisema pajengwe na parekebishwe ili watu wastarehe na fedha zipo lakini  kila siku kunasuasua, msifikiri sioni.

“Saa nyingine mnabishana tu namna ya kumpata mkandarasi mnavutana. Nasikia madiwani mnavutana ninawaomba ndugu zangu sisi wachaguliwa na ninyi wateuliwa ukiwamo mkuu wa mkoa na wakuu wa wilaya  ya shughulikieni miradi  ya Dar es Salaam ikamilike mapema,” amesema Magufuli.

“Nataka miradi ikamilike, naambiwa sasa hivi mkandarasi yupo  anamaliza lini?  akajibiwa na Meya wa Ilala Omar Kumbilamoto kuwa anamaliza mwakani kwa mujibu wa mkataba.