Makonda azungumzia ilani ya CCM, amtaja Magufuli

Muktasari:

  • Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amesema kasi ya utekelezaji wa shughuli za maendeleo inayofanywa na Rais wa Tanzania, John Magufuli inazidi maelekezo ya ilani ya CCM.

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amesema kasi ya utekelezaji wa shughuli za maendeleo inayofanywa na Rais wa Tanzania, John Magufuli inazidi maelekezo ya ilani ya CCM.

Makonda ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Novemba 18, 2019 katika mkutano wake na viongozi wa dini unaofanyika katika ukumbi wa Julius Nyerere (JNICC) ambako anawaeleza mambo yaliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano katika kipindi cha miaka minne.

Amesema kasi ya kiongozi mkuu huyo wa nchi ni kubwa kuliko ilani hiyo, kwamba amefanikiwa kwa kuwa amemtanguliza Mungu mbele.

Amesema uchapakazi huo ndio umewafanya watendaji wengine kumuiga.

“Kawafanya hata viongozi wa Serikali wanaotumia hirizi kumtaja Mungu kwanza. Mara nyingi ameweka wazi kuwa mambo yanavyokwenda kasi hata yeye mwenyewe anamshangaa Mungu,” amesema Makonda.

Amesema ameamua kukutana na viongozi wa dini ili kuwaeleza miradi inayotekelezwa katika Mkoa wa Dar es Salaam.