Marubani wa Tanzania kuwasili na Bombardier, Rais Magufuli kuwapa fedha

Muktasari:

Ndege mpya aina ya Bombardier Q-400 inayotarajiwa kuwasili nchini Tanzania leo Jumamosi Desemba 14, 2019 ikitokea nchini Canada inaendeshwa na marubani Watanzania.

Mwanza. Ndege mpya aina ya Bombardier Q-400 inayotarajiwa kuwasili nchini Tanzania leo Jumamosi Desemba 14, 2019 ikitokea nchini Canada inaendeshwa na marubani Watanzania.

Ndege hiyo kuwasili nchini ikiendeshwa na marubani hao zimeokolewa Sh90 milioni ambazo wangelipwa marubani wa nje.

Akitoa taarifa ya utendaji kwa Rais John Magufuli katika hafla ya kupokea ndege hiyo katika uwanja wa ndege wa Mwanza, mkurugenzi mtendaji wa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL), Ladislaus Matindi amewataja marubani hao Watanzania kuwa ni  Noel Komba na Hamza Ali.

Kutokana na taarifa hiyo, Rais Magufuli ameelezea kufurahishwa na kuagiza marubani hao pamoja na mhandisi wa ndege hiyo mpya kupewa Sh2 milioni kila mmoja.

Akizungumzia mikakati na mpango wa kuwajengea uwezo wataalam wazawa, Matindi amesema shirika hilo la umma limefanikiwa kusomesha na kuajiri marubani wazawa 94 kutoka 11 waliokuwepo mwaka 2016 wakati harakati za kulifufua  shirika hilo uliopoanza.

ATCL ina jumla ya wafanyakazi 521.