Mashine ya Pet CT Scan ya kuchunguza saratani kufungwa hospitali ya Ocean Road

Muktasari:

Mashine nyingine ya kisasa ya kuchunguza saratani kufungwa Ocean Road sambamba na kuanzishwa kiwanda cha dawa za nyuklia

Dar es Salaam. Taasisi ya Saratani ya Ocean Road inatarajia kununua mashine ya Pet CT Scan itakayosaidia kuokoa Sh5 bilioni kwa mwaka ambazo hutumika kuwapeleka wagonjwa nje ya nchi kufuata mashine hiyo.

Mashine hiyo ikifika nchini Tanzania, itakuwa nchi ya kwanza kwa Afrika Mashariki na kati kuwa na kifaa hicho kinachotumika kupima kiwango cha saratani mwilini.

Mkurugenzi wa ORCI Dk Julius Mwaiselage ameyasema hayo leo Desemba 2, 2019 wakati akizungumzia mafanikio ya taasisi hiyo katika miaka minne ya serikali ya awamu ya tano.

Amesema tayari imetoa kiasi cha Sh14.5 bilioni kwa ajili ya mradi utakaohusisha pia ujenzi wa jengo, ununuzi na usimikaji wa kiwanda cha Cyclotron kwa ajili ya kuzalisha dawa za  nyuklia.

Dk Mwaiselage amesema kufikia Aprili 2020 mradi huo utakuwa umekamilika na dawa zitakazozalishwa kwenye kiwanda hicho zitauzwa kwenye hospitali nyingine.

“Mashine ya Pet Scan ikifungwa tutapunguza kiasi cha fedha ambacho ambacho huwa zinatumika kwenda nje ya nchi kupima  na tutawapata wagonjwa kutoka mataifa jirani,”

Pia, Dk Mwaiselage ameeleza kuwa taasisi hiyo imefanikiwa kupunguza idadi ya wagonjwa wanaokwenda nje ya nchi kwa ajili ya matibabu ya saratani.

Amesema mwaka 2019 ni wagonjwa 14 pekee waliopelekwa nje ya nchi kiwango kinachoonekana kupungua ikilinganishwa na 25 wa mwaka 2018 na 164 wa mwaka 2015.