VIDEO: Msomi UDSM aunga mkono hoja ya Kikwete

Muktasari:

  • Msomi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Mohamed Bakari amesema tatizo la viongozi kujikweza linachangiwa na kutokuwa na elimu kuhusu uongozi.

Dar es Salaam. Msomi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Mohamed Bakari amesema tatizo la viongozi kujikweza linachangiwa na kutokuwa na elimu kuhusu uongozi.

Profesa huyo wa Idara ya Sayansi ya Siasa na Utawala Bora chuoni hapo amesema kinachotakiwa ni kutolewa kwa mafunzo ya uongozi kwa viongozi waliopo katika nafasi mbalimbali.

Jana Jumanne Oktoba 8, 2019 Rais wa Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete alitaja sifa alizokuwa nazo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere akisema, “kiongozi ni sawa na mtu mwingine na haikufanyi uwe na haki zaidi kuliko mtu mwingine”.

Katika hotuba yake, Kikwete aliwataka baadhi ya viongozi kuacha utamaduni wa kujikweza akisisitiza unyenyekevu wa kusikilizwa kama ilivyokuwa kwa Mwalimu Nyerere.

“Wengi wanajikweza wakitaka kwenda sambamba na mahitaji ya uongozi uliopo matokeo yake wanajikuta wanakiuka misingi ya utawala bora, kwa sababu unakuta DED (Mkurugenzi) wengi hawajapitia hata public service (utumishi wa umma), tunatakiwa kufahamu kila kitu kinahitaji maandalizi.”

“ Kinachotakiwa ni kutoa mafunzo ya uongozi kwa hao wa ngazi ya chini, wengi hawana mafunzo lakini pia uongozi wa juu unatakiwa kubadilisha utamaduni wake katika staili ya uongozi maana wengi wanaiga wakidhani wanafurahisha uongozi wa juu,” amesema.