Mtunzi wa vitabu Ken Walibora afariki dunia

Muktasari:

Mwandishi wa habari na mtunzi wa vitabu maarufu nchini Kenya, Ken Walibora amefariki dunia leo Jumatano Aprili 15, 2020.

Nairobi. Mwandishi wa habari na mtunzi wa vitabu maarufu nchini Kenya, Ken Walibora amefariki dunia leo Jumatano Aprili 15, 2020.

Walibora aligongwa na gari Ijumaa iliyopita katika barabara ya Landhies mjini Nairobi.

Kwa mujibu wa gazeti la Daily Nation, Walibora hakuonekana tangu Ijumaa na familia yake ilikuwa ikimtafuta kwa siku kadhaa kabla ya kubaini kwamba alikuwa amegongwa na gari.

Walibora ni mmoja wa watunzi mashuhuri wa vitabu nchini Kenya akiwa ameandika takribani vitabu 40.

Baadhi ya vitabu vyake maarufu ni pamoja na Siku Njema ambacho kilitumika kama kitabu cha kiada katika elimu ya sekondari nchini Kenya, na kitabu cha Ndoto ya Amerika.

Pia, alifanya kazi kama msomaji wa taarifa ya habari ya Kiswahili katika kituo cha televisheni cha NTV, kazi ambayo ilimuongezea umaarufu zaidi katika Taifa hilo.

Walibora alipata shahada ya uzamivu ya masomo ya utamaduni katika Chuo Kikuu cha Ohio, huko Marekani.

Pia, alifanya kazi kama profesa msaidizi wa lugha za kiafrika katika Chuo Kikuu cha Wisconsin cha Marekani kabla ya kujiunga na kampuni ya Nation Media Group (NMG) kama msimamizi wa lugha ya Kiswahili, nafasi aliyoitumikia hadi Januari 2017.