Mwili wa Dk Nundu kuzikwa kesho Tanga

Muktasari:

Aliyewahi kuwa mbunge wa Tanga (CCM) na waziri za zamani wa Uchukuzi, Dk Omary Nundu  anasafirishwa kwenda mkoani Tanga kwa ajili ya mazishi  yatakayofanyika kesho Alhamisi.

Dar es Salaam. Mwili wa Mwenyekiti wa Bodi ya kampuni ya simu za mkononi ya Airtel Tanzania, Dk Omary Nundu (71) utazikwa kesho Alhamisi Septemba 12,2019

Dk Nundu aliyewahi kuwa Waziri wa Uchukuzi katika Serikali ya Tanzania iliyopita ya awamu ya nne amefikwa na mauti leo Jumatano Septemba 10, 2019 na mwili wake ulihifadhiwa Hospitali Kuu ya Jeshi Lugola jijini Dar es Salaam.

Maandalizi ya kuusafirisha mwili wa Mwenyekiti huyo wa Bodi ya Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) kwenda mkoani Tanga  zimeanza usiku wa leo Jumatano kwa swala inayofanyika katika Msikiti ni Maamur uliopo Upanga, Dar es Salaam.

Omary Nundu ambaye ni mtoto wa marehemu amesema safari ya kwenda Tanga itaanza saa 4 usiku na wanatarajia mazishi yatafanyika kesho Alhamisi saa 10 jioni.

“Baadhi ya ndugu wataaga kesho na wengine watasindikiza kesho,” amesema Nundu.

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania, Wallace Karia ni miongoni mwa viongozi waliofika msikitini hapo ambapo amesema ni msiba mkubwa kwa watu wa Tanga kwani alikuwa mmoja wa walimu wake wa uongozi.

Karia amesema anamkumbuka Dk Nundu alikuwa mbunge wa Tanga na nafasi mbalimbali za uongozi ikiwemo Uenyekiti wa Bodi ya TTCL na Airtel Tanzania.

“Nimeshirikiana naye akinishauri, ni pengo kubwa na msiba mkubwa kwa watu wa Tanga,” amesema Karia.