VIDEO: Mwili wa bilionea Ali Mufuruki wazikwa Dar

Muktasari:

  • Mfanyabiashara maarufu nchini Tanzania, Ali MUfuruki aliyefariki Desemba 8, 2019 akiwa Afrika Kusini kwa matibabu, mwili wake umezikwa leo Jumanne katika makaburi ya Kisutu, Dar es Salaam.

Dar es Salaam. Mwili wa mfanyabiashara nchini Tanzania, Ali Mufuruki umezikwa leo Jumanne Desemba 10, 2019 katika makaburi ya Kisutu jijini Dar es Salaam.

Mafuruki alifariki dunia usiku wa kuamkia Jumapili Desemba 8, 2019 nchini Afrika Kusini alikopelekwa kwa matibabu.

Maziko wa bilionea huyo Mtanzania yamefanyika saa 10 jioni leo Jumanne na kuhudhuriwa na watu mbalimbali. Kabla ya mwili huo kuzikwa, ulipelekwa ukumbi wa mikutano wa kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam kwa ajili ya ndugu, jamaa na marafiki kuuaga.

Katika makaburi Kisutu mwili uliwasili saa 10:27 ukitokea Msikiti wa Maamur Upanga na kuzikwa saa 10:36.

Baadhi ya viongozi waliokuwapo ni Waziri wa Viwanda na Biashara wa Tanzania, Innocent Bashungwa, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mwananchi Commutations Limited (MCL), Francis Nanai, na Katibu Mkuu mstaafu wa CCM, Abdulrahaman Kinana.

Mufuruki aliyezaliwa Novemba 15, 1958 mkoani Kagera ameacha mjane mmoja Saada Ibrahim na watoto wanne, Laila, Zahra, Sophia na Abdulrazaki.