Nape ampigia kampeni ‘kiani’ Rais Magufuli

Muktasari:

  • Mbunge wa Mtama (CCM), Nape Nnauye amesema ana uhakika kiti chake atakikuta bungeni katika uchaguzi ujao huku akimweleza Rais wa Tanzania, John Magufuli kuwa atapata kura za kutosha katika uchaguzi ujao mwaka 2020.

Dar es Salaam. Mbunge wa Mtama (CCM), Nape Nnauye amemshukuru Rais wa Tanzania, John Magufuli kwa kuridhia kuwapatia Halmashauri ya Wilaya ya Mtama.

Nnauye ametoa shukrani hizo leo Jumanne Oktoba 15, 2019 wakati wa ziara ya kikazi ya Rais Magufuli katika mkoa wa Lindi.

“Siwezi kupata maneno mazuri kutosha kukushukuru, nikuahidi jambo moja, kwetu sisi wewe umemaliza kazi, kazi iliyobaki ni kwetu kwenye serikali za mitaa, mwakani kwa madiwani,” amesema Nnauye

“Jimbo la uchaguzi wangu umemaliza kabisa kiti changu pale bungeni na hakika nitakikuta lakini kura zako safari hii Rais tudai za kutosha,” amesema waziri huyo wa zamani wa habari, utamaduni, sanaa na michezo

Amesema mkoa huo ulipoteza majimbo manne mwaka 2015, wamefanikiwa kurejesha jimbo moja na mengine yatarejea katika uchaguzi ujao mwaka 2020.

Amesema licha ya kujenga halmashauri hiyo, Serikali ilitoa Sh2.8 bilioni kwa ajili ya afya, Sh3.8 kwa ajili ya maji na Sh24 milioni kwa ajili ya miradi ya umeme.

 Amesema fedha hizo ni ushahidi tosha kwamba Serikali ya awamu ya tano imeamua kusimamia ipasavyo makusanyo, matumizi na ndio maana fedha zimepatikana na miradi inaendelea.