Ndugai amzulia jambo Zitto kuhusu Sh1.5 trilioni

Muktasari:

Spika Job Ndugai amemtaka mbunge wa Kigoma Zitto Kabwe kuwa na hofu ya Mungu na aache uongo kuhusu sakata la Sh1.5 trilioni


Dodoma. Spika Job Ndugai amedai mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalenmdo), Zitto Kabwe ni muongo kwa maelezo kuwa amekuwa akizungumza habari zisizo za kweli dhidi yake.

Akizungumza bungeni leo Alhamisi Januari 31, 2019 Ndugai amesema licha ya uongo huo ni mapema mno kumpeleka kiongozi huyo wa ACT katika Kamati ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge.

Amesema Zitto amekuwa akiandika kwenye mitandao ya kijamii kuhusu Ndugai kuikalia ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuhusu upotevu wa Sh1.5 trilioni,  jambo ambalo si kweli.

Ndugai amebainisha kuwa taarifa za mbunge huyo kwenye mitandao ya kijamii hazina ukweli na ni uongo mtupu: ”Siwezi kufumbia macho kiasi hicho cha fedha kipotee bure.

“Kwa mfano, aliandika katika mtandao wake kuwa nilipokea ripoti ya CAG tangu Januari 8, 2019 nikaikalia wakati mimi nimepokea taarifa hiyo Januari 16, 2019 na Januari 18, 2019 niliwapa kamati ya PAC. Ni vyema Watanzania wakajua huyu mwenzetu ni muongo,” amesema Ndugai.

Amesema Bunge liliweza kujadili habari za Sh300 bilioni kwa nguvu iweje washindwe kujadili kuhusu Sh1.5 trilioni ambazo ni nyingi.

Hata hivyo, amesema CAG, Profesa Mussa Assad alishaulizwa mbele ya Rais John Magufuli kuhusu fedha hizo na kubainisha kuwa hakuna upotevu wa kiasi hicho na hata kamati ya PAC ilishasema hakuna upotevu, lakini anashangaa kuona Zitto analisambaza jambo hilo.