Ndugai awapoza wabunge miradi ya maji, aishauri Serikali
Muktasari:
Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai amesema kero ya kutokamilika kwa miradi ya maji ni ya wabunge wengi na kuitaka Serikali kushauri namna ya kushughulikia suala hilo kabla ya kuvunjwa kwa Bunge la 11.
Dodoma. Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai amesema kero ya kutokamilika kwa miradi ya maji ni ya wabunge wengi na kuitaka Serikali kushauri namna ya kushughulikia suala hilo kabla ya kuvunjwa kwa Bunge la 11.
Ndugai ametoa kauli hiyo leo Jumanne Septemba 3, 2019 wakati akijibu mwongozo wa mbunge wa Mpwapwa (CCM), George Lubeleje aliyesema miradi ya maji inachukua hadi miaka minne kukamilika wakati inatumia fedha za ndani.
“Waziri wa maji atoe kauli hapa bungeni kwa nini miradi ya maji inachukua miaka mitano hadi sita haikamiliki naomba mwongozo wako mheshimiwa Spika,” amesema.
Akijibu Ndugai amesema Serikali imelisikia na watatazama namna ya kuwashauri, akisisitiza kuwa suala hilo ni kero inayowagusa wabunge wengi.
“Wakati tunaelekea kwenye kimbembe maana bado mikutano mitatu tu (Kabla ya kuvunjwa kwa Bunge la 11). Serikali itatushauri namna gani ya kuendana na jambo hili,” amesema Ndugai.