Profesa Kabudi ataja sababu kuambatana na Magufuli

Muktasari:

Waziri wa Mambo ya Nje nchini Tanzania,  Profesa Palamagamba Kabudi ameweka  wazi sababu za kuambatana na Rais John Magufuli katika ziara zake huku akiwataka Watanzania kuzoea hali hiyo.

T: Profesa Kabudi ataja sababu kuambatana na Magu

Dar es Salaam. Waziri wa Mambo ya Nje nchini Tanzania,  Profesa Palamagamba Kabudi ameweka  wazi sababu za kuambatana na Rais John Magufuli katika ziara zake huku akiwataka Watanzania kuzoea hali hiyo.

Akizungumza leo Jumatatu Oktoba 7, 2019 katika uzinduzi wa mradi wa maji mkoani Rukwa,  Profesa Kabudi amesema kushiriki kwenye ziara hizo kunamuwezesha kufanya kazi zake kwa ufanisi.

“Mimi ni tofauti mtaniona kwenye shughuli za hapa ndani mara nyingi zaidi, nitakuwa kwenye ziara kama hizi na rais ili kuona maendeleo ya Watanzania ninapokuwa huko nje nieleze mambo niliyoyaona na kuyashuhudia.”

“Huwezi kuwa waziri wa mambo ya nje kwa ufanisi kama huhudhurii shughuli hizi, utaacha kuwawakilisha watanzani au kuwasema watanzania utaanza kuwazungumzia hao unaowafuata huko nje. Watanzania hawakuzoea kuona waziri wa mambo ya nje yupo kwenye shughuli hizi,” amesema Kabudi.

Profesa Kabudi amesema aliumizwa na maelekezo ya rais yaliyomtaka kushiriki kwenye ziara nchini lakini sasa ameanza kuona matunda yake.

“Mara baada ya kuniteua uliniambia mimi ni waziri wa watanzania, nilinyong’onyea kidogo baada ya kuona kwamba nitakuwa sana nchini badala ya kupaa nje lakini sasa naona faida yake,” amesema