Safari za ATCL mkoani Katavi zazinduliwa

Muktasari:

  • Rais wa Tanzania, John Magufuli leo Jumamosi Oktoba 12, 2019  amezindua safari za Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kutoka Dar es Salaam kwenda mkoani Katavi.

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, John Magufuli leo Jumamosi Oktoba 12, 2019  amezindua safari za Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kutoka Dar es Salaam kwenda mkoani Katavi.

Mbali na uzinduzi huo, Magufuli ameipongeza ATCL kwa kuanzisha safari hizo kwa kuwa zitachochea biashara na utalii katika mikoa ya karibu na Katavi na nchi za DRC Congo na Zambia.

Katika uzinduzi huo uliofanyika mkoani Katavi, Magufuli amesema, “ATCL liendelee kutoa huduma nzuri kwa Watanzania na muendelee kuzingatia muda.”

“Mkisema mtafika muda fulani uwe muda huo. Mnapokosa mtoe taarifa mapema. Muangalie vizuri gharama zenu ili Watanzania wafaidike na ndege hizi.”

Awali  akitoa taarifa kuhusu safari hizo, mkurugenzi wa ATCL, Ladislaus Matindi amesema kutakuwa na safari moja ya Dar es Salaam kwenda Mpanda.

“Hiyo safari itakuwa Jumatano na ndege ndege itatoka Dar es Salaam kwenda Mpanda ikipitia Tabora itakayochukua saa mbili wakati wa kwenda.”

“Ombi letu si Mpanda tu na Rukwa, kuna nchi za jirani katika huu mkoa. Kwa hiyo tuhamasishe nchi jirani kama Zambia, DRC na Burundi. Tufanye kazi pamoja kwa kujua huu ni uwekezaji wenu na ni kodi zenu mafanikio yake ni mafanikio yenu,” amesema Matindi.

Matindi amesema ikifika Novemba, 2019 wataongeza safari kufikia tatu kwa kuzingatia ongezeko la abiria.

Katika hatua nyingine, Rais Magufuli amesema kuna ndege nyingine moja inayoendelea kutengenezwa nchini Marekani  na itawasili nchini mwishoni mwa mwaka 2019 itakayokuwa na uwezo wa kubeba abiria 262.

Mbali na ndege hiyo amesema kuna ndege nyingine tatu zinaendelea kutengenezwa.

“Tunataka Tanzania mpya ya kisasa watu wafanye biashara wazunguke wanavyotaka watengeneze pesa,” amesisitiza Magufuli.