Ujenzi reli ya kisasa Dar- Morogoro wafikia asilimia 42

Mkurugenzi mtendaji wa Shirika la Reli nchini (TRC), Masanja Kadogosa

Muktasari:

  • Mkurugenzi wa Shirika la Reli nchini (TRC), Masanja Kadogosa amesema ujenzi wa reli ya kisasa unaendelea vizuri na sasa umefikia asilimia 42 kwa kipande cha Dar es salaam hadi Morogoro.

Dar es Salaam.  Mkurugenzi mtendaji wa Shirika la Reli nchini (TRC), Masanja Kadogosa amesema ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) umefikia asilimia 42 kwa kipande cha Dar es Salaam Morogoro wakati kipande cha Morogoro - Matukupora kikifikia asilimia sita.

Akizungumza na Mwananchi leo Jumatatu Februari 11, 2019 Kadogosa amesema ujenzi huo unaendelea vizuri na wanatarajia kumaliza ndani ya muda wa miezi 10 iliyobaki kwa mujibu wa mkataba wa ujenzi.

"Ukisikia asilimia 42 unaweza ukadhani ni chache sana, kazi kubwa iko kwenye civil ambayo ni asilimia 60 ya kazi yote. Kati ya hizo asilimia 60, tumefikia asilimia 42," amesema mkurugenzi huyo.

Kadogosa amebainisha kwamba kipande cha Morogoro - Matukupora nacho ujenzi unakwenda vizuri na sasa wamefikia asilimia sita. Amesema kwa ujumla kazi inakwenda vizuri na wataendelea kusimamia mkataba wao na mkandarasi.

Amesema treni ya SGR itakuwa na uwezo wa kusoma alama mbalimbali ambazo zitawawezesha wasimamizi kujua mahali penye hitilafu na kwenda moja kwa moja kurekebisha.

"Tutakuwa na ex ticket, tracking system na mfumo wa mawasiliano ambao utamwezesha dereva kuona treni zote zilipo, hivyo hakutakuwa na haja ya kusubiriana kama tunavyofanya sasa kwenye treni yetu," amesema mkurugenzi huyo.