VIDEO: Makonda asema aibu waliyoipata viongozi wa Dar isijirudie

Muktasari:

  • Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Paul Makonda ameagiza miradi yote katika mkoa huo ikamilike kabla ya uchaguzi Mkuu ujao mwaka 2020 huku akikemea watendaji kujihusisha na rushwa katika miradi hiyo

Dar es salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda ameagiza miradi yote katika mkoa huo ikamilike kabla ya uchaguzi mkuu ujao 2020.

Makonda ametoa kauli hiyo leo Jumatano Septemba 25,2019 jijini Dar es Salaam wakati wa kikao cha uchambuzi wa miradi ya maendeleo iliyokwama katika jiji hilo.

Wakuu wa wilaya za Ubungo, Kinondoni, Ilala, Temeke, Kigamboni pamoja na Jiji hilo wamewasilisha taarifa za utekelezaji wa miradi iliyokwama na iliyokamilika,  yenye thamani ya takribani Sh3trilioni.

"Ukiangalia kwa ujumla ni kama miradi yote imekamilika kwa asilimia 75 hadi 80, wako wanaofanya vizuri lakini wengine ukienda field, hadi kufikia Mei mwakani miradi yote iwe imekamilika, " amesema Makonda.

"Tujenge timu ya matokeo chanya, kila mmoja atambue upungufu aliyonayo katika nafasi yake, aibu tuliyoipata tusipate tena."

Mkutano huo umehusisha Wakurugenzi, Wakuu wa wilaya, watendaji, wakandarasi, Maofisa wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) na Wakala wa Barabara Mjini na Vijijini (Tarura) pamoja na viongozi wa CCM ngazi ya wilaya na mkoa.

Baadhi ya masuala yaliyoibuliwa ni pamoja na watendaji kutengeneza mazingira ya rushwa na baadhi ya maofisa kukwamisha miradi Kwa kigezo cha taratibu za kazi.