WCB yapata kigugumizi kumzungumzia Harmonize

Muktasari:

Lebo ya WCB imesema haipo tayari kwa sasa kuzungumza lolote kumhusu msanii aliyekuwa katika lebo hiyo, Rajabu Abdul Kahali maarufu Harmonize ikiwa ni wiki chache tangu taarifa za msanii huyo kuondoka ndani ya lebo kusambaa.

Dar es Salaam. Huku na huku hakuna anayejua ukweli kuhusu msanii aliyeunda lebo ya WCB, Rajabu Abdul Kahali maarufu Harmonize, baada ya taarifa zake za kuondoka katika lebo hiyo aliyodumu nayo kwa miaka kadhaa.

Harmonize ambaye umaarufu wake ulikua na kusikika ndani na nje ya nchi alipokuwa ndani ya lebo hiyo, hivi karibuni amezua gumzo mitandaoni baada ya taarifa za yeye kutoka huku mashabiki wakibaki kujiuliza maswali lukuki kuhusu kuvunjwa kwa mkataba wake.

Mwananchi Digital Jumatatu Oktoba 21, 2019 imefanya mahojiano na mmoja wa mameneja wa lebo hiyo Hamis Taletale maarufu Babu Tale ikitaka kujua undani wa taarifa hizo.

Hata hivyo baada ya mahojiano ya muda mrefu kuhusu tuzo ya meneja bora Afrika aliyoipata jana Jumapili kupitia tuzo za African Entertainment Awards USA 2019, Babu Tale aliruka kimanga kujibu maswali aliyoulizwa.

 

Mwandishi: Umekuwa meneja kwa miaka mingi na umeongoza wasanii wengi, kuna hili suala la Harmonize kutoka lebo ya WCB unalizungumziaje?

 

Babu Tale: Hiyo issue iko hivyohivyo na siwezi kuijibu.

 

Mwandishi: Kuna taarifa kuwa amelipa kiasi cha fedha na inashindikana bado kujitoa hili lipoje?

 

Babu Tale: Siijui. Siwezi kujibu.