Wachezaji washikilia kibarua cha Solskjaer Man United

Muktasari:

Kibarua cha kocha wa Manchester United, Ole Gunnar Solskjaer kipo mikononi mwa wachezaji wa timu hiyo katika mchezo dhidi ya Liverpool.


London, England. Kocha Ole Gunnar Solskjaer amesema ameingia hofu ya kupoteza kazi Manchester United endapo watafungwa na Liverpool.

Man United na Liverpool zitavaana Oktoba 20 katika mchezo wa Ligi Kuu England, utakaochezwa Uwanja wa Anfield.

Solskjaer ametoa kauli hiyo akiwa na maumivu ya kufungwa bao 1-0 dhidi ya Newcastle United katika mchezo uliopita.

Makamu Mwenyekiti na Mtendaji Mkuu wa Man United, Ed Woodward hajatoa tamko kuhusu hatima ya kocha huyo licha ya kufanya vibaya msimu huu.

Kocha huyo alisema njia pekee ya kunusuru kibarua chake ni kupata ushindi dhidi ya watani wao wa jadi.

Man United ilifungwa mabao 3-1 kwenye uwanja huo Desemba mwaka jana na matokeo hayo yalichangia kumng’oa Jose Mourinho.

Licha ya kujaza nafasi ya Mourinho akianzia nafasi ya kocha wa muda kabla ya kupewa mkataba Machi, Solskjaer ameshinda mechi tano kati ya 21.

Matokeo mazuri aliyopata nguli huyo wa zamani wa Norway ni ushindi mnono wa mabao 4-0 dhidi ya Chelsea katika mchezo wa ufunguzi wa Ligi Kuu Agosti, mwaka huu.