Waliofukiwa na kifusi wafikisha siku ya sita, changamoto ya kuwaokoa yatajwa
Muktasari:
Juhudi za kuwaokoa watu wawili waliofukiwa na kifusi katika mgodi wa Imalanguzu wilayani Geita tangu Oktoba Mosi, 2019 zimekwama kutokana na njia iliyokuwa ikitumika kuwafikia kuwa na magogo makubwa yanayohatarisha usalama wa waokoaji.
Geita. Juhudi za kuwaokoa watu wawili waliofukiwa na kifusi katika mgodi wa Imalanguzu wilayani Geita tangu Oktoba Mosi, 2019 zimekwama kutokana na njia iliyokuwa ikitumika kuwafikia kuwa na magogo makubwa yanayohatarisha usalama wa waokoaji.
Kutokana na changamoto hiyo wachimbaji wadogo waliokuwa
wakitoa udongo na kuimarisha njia kwa kuweka magogo wamerejesha jukumu hilo kwa Serikali iliyoanza kutoa udongo kwa kutumia Katapira.
Shija Robert, mmoja wa wachimbaji wadogo katika eneo hilo amesema uwezo wao umefika mwisho na sasa wameiachia Serikali ione njia ya kufanya kuwaokoa wachimbaji hao.
Kamishna msaidizi mwandamizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji mkoani Geita, Zablon Mhumha amesema “kwa sasa tunatumia Katapira kutafuta njia pembeni kutokana na njia ya awali kuwa hatari.”
Amesema wachimbaji wadogo walitoa udongo hadi umbali wa mita 50 lakini kutokana na ukubwa wa magogo yaliyoko ndani imekua ngumu wao kuendelea.
“Kwa sasa Katapira inatoboa njia nyingine ili kuona namna ya kuokoa wachimbaji hao ambao wako chini kwa siku sita sasa,” amesema Mhumha.