Wosia wa bilionea aliyeuawa Kenya wafunguliwa

Muktasari:

  • Mke wa bilionea huyo kupitia wakili wake amekataa kuutambua wosia huo.

Nairobi, Kenya. Wosia ulioachwa na bilionea Tob Cohen umewekwa hadharani mbele ya familia yake.

Wosia huo ulifunguliwa jana Ijumaa Septemba 20 mbele ya wanafamilia na marafiki wa bilionea huyo jijini Nairobi.

Hata hivyo, mke wa mfanyabishara huyo, Sarah Wairimu ambaye kwa sasa anashikiliwa kwa tuhuma za kuhusika na mauaji ya mumuwe kupitia wakili wake alikataa kuutambua wosia huo na kusema kuwa ni batili.

Aprili mwaka huu Sarah na bilionea Cohen walifungua kedi ya talaka ambako hata hivyo, haikuamuriwa mpaka mpaka mfanyabishara huyo alipopoteza maisha.

Mapema jana asubuhi wakili wa mfanyabishara huyo, Chege Kirundi, ambaye ndiyo msimamizi wa wosia huo aliwaambia waandishi wa habari kwamba yaliyomo katika wosia huo yatabaki ya binafsi isipokuwa kama familia ya Cohen itaagiza vingine.

"Hatutajadili maelezo yoyote yaliyomo kwenye wasioa huo kwa wakati huu,” alisisitiza wakili Kirundi na kuongeza kuwa wosia huo utasomwa wakati suala hili litakapofika mahakamani kwa ajili ya kusikilizajwa

Kwa upande wake wakili Cliff Ombeta, anayemwakilisha dada wa bilionea huyo, Gabrielle Van Straten alisema mawakili wa Sarah walialikwa kwenye hafla hiyo lakini walikataa kwa maelekezo kutoka kwa mteja wao.

"Tulimwalika Sarah lakini hajafika. Tumewasubiri kwa muda mrefu lakini hawajafika wala hawakutuma mwakilishi,” alisisitiza wakili huyo.

Hata hivyo, familia ya mfanyabishara huyo akiwamo kaka yake Bernard waligoma kuzungumza na waandishi wa habari kuhusu taarifa zaidi za wosia huo.

Marehemu Cohen imeacha kiasi kikubwa cha fedha katika akaunti za benki, hisa katika kampuni mbalimbali na mali isiyohamishika.