CAG abaini udhaifu usimamizi wa urejeshaji mikopo kwa wasanii
Muktasari:
- Ripoti hiyo ya mwaka wa fedha wa 2024/2025 ilibaini kuwa TACAF ilitoa mikopo kwa wasanii 45 kati ya Desemba 2022 na Februari 2023 lakini hadi kufikia Novemba 2025, jumla ya Sh765.94 milioni zilikuwa hazijalipwa na wasanii 40.
Dar es Salaam. Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) imebaini mapungufu katika usimamizi wa mikopo ya riba nafuu, inayotolewa na Mfuko wa Utamaduni na Sanaa Tanzania (TACAF) kwa lengo la kuimarisha sekta ya ubunifu na kuongeza ushindani wa wasanii.
Ripoti hiyo ya mwaka wa fedha wa 2024/2025 ilibaini kuwa TACAF ilitoa mikopo kwa wasanii 45 kati ya Desemba 2022 na Februari 2023 lakini hadi kufikia Novemba 2025, jumla ya Sh765.94 milioni zilikuwa hazijalipwa na wasanii 40.
Kati yao, wasanii saba walikuwa hawajaanza kabisa kurejesha mikopo hiyo. CAG anabainisha kuwa mikopo hiyo ilitolewa bila dhamana, jambo ambalo limeongeza hatari ya mfuko kupoteza fedha na kudhoofisha uendelevu wake.
Aidha, kutokana na TACAF kutokuzingatia ushauri wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali wa kurekebisha makubaliano ya dhamana na benki. Benki husika ilikata kiasi cha Sh88.32 milioni moja kwa moja kutoka kwenye akaunti ya mfuko tarehe 19 Desemba 2024 ili kufidia mikopo isiyolipwa.
Ripoti hiyo inaeleza licha ya hasara hiyo, uongozi wa mfuko haukuchukua hatua zozote za kisheria au za ukusanyaji dhidi ya wasanii walioshindwa kulipa.