Madiwani wahoji ujenzi hospitali ya wilaya kukwama

Muktasari:

Madiwani wa  halmashauri Mtama mkoani Lindi wamekerwa na kitendo cha Sh500 milioni  kutotosha katika ujenzi wa wodi tatu za hospitali ya wilaya



Lindi. Madiwani wa halmashauri Mtama mkoani Lindi wamekerwa na kitendo cha Sh500 milioni kutotosha katika ujenzi wa wodi tatu za hospitali ya wilaya.

Kutotosha kwa fedha hizo kumeelezwa na  mhandisi  idara ya ujenzi, Abruhan  Juma  kutoa taarifa ya  kuchelewa kukamilika kwa ujenzi  wa wodi ya uzazi, wanaume na wanawake kwamba umekwama kwa sababu kiasi hicho  cha fedha kuisha na kuhitajika nyingine Sh198 milioni.

"Mradi umesimama baada ya  ongezeko la mahitaji ya vifaa ikiwemo mbao na silingi bodi," amesema Juma.

Madiwani Halmashauri ya mtama mkoani Lindi

Akizungumza kwa niaba ya madiwani, diwani wa Nahukahuka,  Hamza Nguachi amesema  wanatambua Serikali imepeleka Sh500  milioni lakini cha kushangaza hazikutosha," fedha hizi zimepelekwa kila wilaya kwa maelekezo lakini kwingine zmemaliza ujenzi ila Mtama zimeshindwa kukamilisha ujenzi na kunahitajika nyingine kama Sh200 milioni," amesema Nguachi

Diwani mwingine, Hawa Nameta amesema uadilifu kwa watendaji umekuwa mdogo kwani wamekuwa wakijali maslahi yao binafsi kuliko halmashaur hali ambayo isipo zibitiwa itaendelea kudidimiza maendeleo ya halmashauri.

"Siku mmoja nilitamani kulia nliipoambiwa kuna vifaa  vya ujenzi vinatakiwa kununuliwa nje ya halmashauri ya Mtama wakati vinapatikana kila mahali hapa tena kwa bei ya kupatana," amesema  Nameta

Rashidi Mega, mwenyekiti wa kijiji cha Kiwalala amesema kitendo cha madiwani kuhoji  na kutokubaliana kuongeza fedha za kumalizia mradi wa ujenzi wa wodi tatu  ni sahihi kwani miradi ya Serikali inaletwa kwa bajeti na maelekezo.

"Kwanza niwapongeze madiwani wangu kwa kuwa na msimamo wa namna hiyo wakiendelea na tabia hiyo watarudisha uaminifu, uwajibikaji na uadilifu kwa watendaji," amesema  Mega.

Mkurungezi mtendaji wa halmashauri hiyo,  George Mbilinyi amesema wana changamoto nyingi ikiwemo matumizi ya fedha bila kufuata utaratibu, miradi kutokamilika kwa wakati.

"Ndugu zangu hii halmashauri inakosa  usimamizi kila mtumishi alikuwa anafanya kazi kivyake na kimazoea  kulikuwa hakuna wa kusimamia hayo,  nimewaomba madiwani  kunipa muda kurudisha nidhamu kazi, uadilifu na mahusiano," amesema Mbilinyi.