Benki ya Exim yakamilisha umiliki wa benki ya FNB, yawapokea wateja wapya

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Exim Tanzania Jaffari Matundu akizungumza na wageni waalikwa kwenye hafla fupi ya kuwakaribisha wateja wa iliyokuwa Benki ya FNB Tanzania waliohamia benki ya Exim kufuatia benki hiyo kuinunua iliyokuwa benki ya FNB Tanzania ikiwa ni muendelezo wa mkakati wake wa kujitanua zaidi ndani na nje ya mipaka ya nchi.

Dar es Salaam. Benki ya Exim Tanzania imetangaza rasmi kuinunua iliyokuwa Benki ya FNB Tanzania ikiwa ni muendelezo wa mkakati wa benki hiyo kujitanua zaidi ndani na nje ya mipaka ya nchi. Hii ikiwa ni chini ya miaka mitatu tu tangu iliponunua benki ya UBL Tanzania.

Akizungumza kwenye hafla fupi ya kuwakaribisha wateja wa iliyokuwa Benki ya FNB Tanzania iliyofanyika jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Exim Tanzania, Jaffari Matundu alisema hatua hiyo imekuja kufuatia kukamilika kwa mafanikio makubwa kwa mchakato wa umiliki wa benki hiyo chini ya uangalizi wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT)

Akizungumza kwenye hafla hiyo mmoja wa wateja wa iliyokuwa benki ya FNB Tanzania  Amandus Manda (pichani) aliwatoa hofu wateja wenzake wanaohamia benki ya Exim huku akiwataka wawe na imani na huduma zinazotolewa na benki hiyo iliyowekeza zaidi kwenye utoaji wa huduma zake kidigitali.

“Ununuzi wetu wa Benki ya FNB Tanzania unatuwezesha kuongeza idadi ya wateja watakaofikiwa na huduma za benki ya Exim ndani na nje ya nchi. Tukiwa tunaelekea kuadhimisha miaka 25 ya kuanzishwa kwa benki hii, tunajivunia ukuaji huu unaotupa hadhi ya kuwa benki kimbilio si tu Tanzania bali pia nje ya nchi ambapo pia tunaendelea kujitanua’’ alisema.

Hafla hiyo iliyohudhuliwa na wateja wapya wa benki ya Exim kutoka iliyokuwa Benki ya FNB Tanzania, wafanyakazi wa benki wa Benki ya Exim pamoja na wawakilishi kutoka mamlaka mbalimbali zinazosimamia sekta ya fedha hapa nchini.

Mbali na Tanzania benki hiyo pia ina matawi yake katika nchi za Uganda, Djibouti, Comoros na Ethiopia.

Mpaka sasa, benki ya Exim iko miongoni mwa benki tano bora nchini yenye mali za tabriban Sh 2.4 trilioni kwa ujumla katika nchi zote 4.

Benki ya Exim ndani ya mwaka huu, katika kipindi cha nusu ya kwanza, imeendelea kufanya vizuri sokoni kwa kuzalisha faida ya kabla ya kodi ya Sh 18 bilioni ikilinganishwa na Sh 6 bilioni iliyopatikana katika nusu ya kwanza mwaka jana. Ukuaji wetu wa jumla ya mali hadi Sh 1.5 trilioni kutoka Sh 1.3 trilioni mwaka uliopita na dhamana za wateja kutoka Sh 780 Bilioni Juni mwaka jana hadi Sh 943 bilioni Juni mwaka huu.

Benki iliweza kufanya vizuri, kwanza kutokana na mazingira mazuri yaliyowekwa na Serikali na pili, kuzindua huduma na bidhaa mbalimbali za kibenki zikiwemo Bima ya Exim, Exim Wakala na nyingine nyingi ambazo kwa pamoja zimeendelea kuiweka karibu na jamii na kuiruhusu kuendelea kutoa huduma bora za kibunifu na za uhakika katika kipindi chote.

“Tupo hapa leo kuwahakikishia wateja wetu wapya kuwa tunafurahi kuwa nao kwenye safari yetu na tutaendelea kujitoa kwa dhati kabisa kuhakikisha kwamba wanaendelea kufurahia huduma zenye ubunifu zaidi. Wateja wakiwa ni sehemu muhimu zaidi ya biashara yetu, tunaahidi kufanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha wanafurahia huduma zetu zinazotelewa kidigitali zaidi,’’ alisema.

Aidha Matundu alitumia fursa hiyo kuishukuru serikali kwa namna inavyoendelea kwa kujenga, mazingira wezeshi ya kufanya biashara kupitia sera nzuri zinazochochea ukuaji wa biashara hatua ambayo imechochea ukuaji wa taasisi mbalimbali za kifedha hapa nchini.

Akizungumza kwenye hafla hiyo iliyohudhuliwa na wateja, wafanyakazi wa benki ya Exim pamoja, na wawakilishi kutoka mamlaka mbalimbali zinazosimamia sekta ya fedha hapa nchini. Mmoja wa wateja wa iliokuwa benki ya FNB Tanzania Amandus Manda aliwatoa hofu wateja wenzake wanaohamia benki ya Exim huku akiwataka wawe na imani na huduma zinazotolewa na benki hiyo iliyowekeza zaidi kwenye utoaji wa huduma zake Kidigitali.

“Kabla ya hatua hii mimi na kampuni yangu tulikuwa tunapata huduma zetu za kibenki kutoka kwa benki zote mbili yaani Benki ya FNB pamoja na benki ya Exim. Katika kipindi chote nilichokuwa napata huduma za Exim sikuwahi kutembelea tawi lao wala kuonana na ofisa yeyote wa benki hii hata siku moja kwa kuwa huduma zote nilikuwa nazipata kwa njia ya kidigitali. Kwa hiyo niwahakikishie wenzangu tupo mikono salama zaidi,’’ alisema