Saccos 400 hazijakidhi vigezo

Dar es Salaam. Kamisheni ya Tume ya Maendeleo ya Ushirika (TCDC) imesema kati ya vyama 1,183 vya ushirika vya akiba na mikopo (Saccos) vilivyoomba leseni nchini, 789 vimekidhi vigezo kulingana na Sheria ya Huduma Ndogo ya Fedha.

Kauli hiyo ilitolewa juzi na Mrajis na mkurugenzi mtendaji wa TCDC, Dk Benson Ndiege katika mkutano wa sita wa Jukwaa la Ushirika la Mkoa wa Dar es Salaam, akibainisha kuwa kuna Saccos 386, zimeelekezwa kuboresha taarifa zake ili kupata leseni.

Mkutano huo, ulikuwa na lengo la kujitathimini kwa kujadili mafanikio, changamoto na kuweka mikakati ya kusonga mbele kwa maendeleo ya jukwaa hilo.

“Katika daftari letu kuna vyama 3,000, maana vyama 2,000 havijaomba kabisa, kwa Mkoa wa Dar es Salaam, vilivyopata leseni ni 200 kati ya 500. Kwenye majadailiano yenu ningeomba mjadili suala la kupata leseni kwa ajili ya shughuli hii.

“Tumetoa muda kidogo hadi Mei 30 mwaka huu, kila chama cha ushirika kiwe kimemaliza kujisajili na kuomba leseni. Tunataka hadi Mei 30 mwaka huu, vyama vyote 500 viwe vimeomba leseni,” alisema Dk Ndiege.

Hata hivyo, Ndiege alisema TCDC imeweka mpango mzuri wa kuvilea ili wvyama visivyopata leseni vizipate, akisema vitapewa hadi mwaka mmoja kulingana na maombi ya chama husika.

Mwenyekiti wa Jukwaa la vyama vya ushirika la mkoa wa Dar es Salaam, Mussa Chowa alisema wanakabiliwa na changamoto ya kodi ya mapato inayotozwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), akisema kodi hizo zinasababisha gharama kubwa za uendeshaji wa vyama.

“Jambo hili linapunguza faida kwa vyama vya ushirika na kusababisha wanachama kutoona faida za vyama vya ushiriki,” alisema Chowa.

Mwenyekiti wa TCDC, Abdulmajid Nsekela aliwaahidi wanajukwa la ushirika la mkoa huo, kushughulikia changamoto zinazowakabili, huku akitaka zile zilizopo ndani ya uwezo wao wazifanyie kazi.