Bodi yawapoka chama kina Hamad Rashid
Mwenyekiti wa Bodi ya wadhamini wa Chama cha ADC, Kimangale Ayoub Juma (kushoto), akiwa na Makamu Mwenyekiti wa bodi hiyo, Khamis Juma Shoka wakizungumza na waandishi wa Mwananchi kwenye ofisi za chama hicho, Buguruni, Dar es Salaam jana.
Picha na Anthony Siame
Muktasari:
Akizungumza jana mjini Dar es Salaam, Miraj alisema bodi hiyo haijitambui kwa kuwa inafanya mambo kinyume na katiba yao inavyoelekeza.
Dar es Salaam. Mgogoro kati ya Mwenyekiti wa Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC), Said Miraj na mlezi wa chama hicho, Hamad Rashid Mohamed umechukua sura mpya baada ya bodi ya wadhamini kuamua kuchukua mamlaka ya kukiendesha chama hicho.
Hatua hiyo imelalamikiwa na Miraj na amesema tayari wamemwandikia barua Msajili wa Vyama vya Siasa kuhusu sakata hilo la kuondolewa madarakani kuwa imefanywa kinyume na katiba ya chama chao.
Akizungumza jana mjini Dar es Salaam, Miraj alisema bodi hiyo haijitambui kwa kuwa inafanya mambo kinyume na katiba yao inavyoelekeza.
“Ni dhahiri kwamba wajumbe wa Bodi ya ADC wanasukumwa na utashi wao binafsi hivyo wameamua kutupora madaraka ili watimize malengo yao kwa kisingizio cha hoja tofauti zilizopo kati ya mlezi wa chama, Hamad Rashid na mimi Miraj,” imeeleza sehemu ya barua iliyoandikwa kwenda kwa msajili.
Miraj alisema Hamad Rashid ni mwanachama wa kawaida hawezi kupewa uongozi wakati bado hajafikisha miezi sita kwa mujibu wa katiba yao, lakini ameshangazwa na kuona ‘akijitwisha’ madaraka kinyume cha katiba.
“Tulitakiwa kukutana na bodi hiyo Januari 11, (juzi), kwa lengo la kujadili kwa pamoja na mapato na matumizi, fedha zilizotumika pamoja, miradi ya ADC na ufuatiliaji wa fedha zingine, lakini tunashangaa kuona kazi hiyo ikifanywa na bodi ya wadhamini ambayo siyo kazi yake, ilipaswa ifanywe na bodi ya uongozi wa kitaifa,” alidai Miraj.
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Bodi ya ADC, Kimangale Mussa alisema wamelazimika kuchukua hatua hiyo baada ya kuona uongozi uliopo ukikosa nidhamu na kuamua kujadiliwa mambo yanayokihusu chama kwenye vyombo vya habari.
“Tumefuata katiba inavyoelekeza, tutashika madaraka haya kwa mwezi mmoja, huku tukiendelea kujadiliana na kuangalia namna ya kuupata uongozi mwingine tutakaouweka madarakani,” alisema Mussa.
Alisema bodi inao ushahidi wa kutosha unaonyesha namna kamati hiyo ya utendaji ilivyoshindwa kufanya kazi na kusababisha chama kukosa diwani hata mmoja katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwaka jana.