R Kelly adai kutumwa na mizimu

Muktasari:

  • Inadaiwa anaiamini katika kufanya maamuzi kuliko hata  wasaidizi wake

New York, Marekani. Moto umezidi kumuwakia mwanamuziki R Kelly ambaye sasa imeelezwa kuwa amegeukia mizimu akidai kuwa imekuwa ikimsukuma kufanya maamuzi.

R Kelly ambaye amekuwa katika misukosuko ya tuhuma za kutumikisha kingono mabinti na za kutelekeza watoto wake, amesema alifanya mahojiano na kituo cha CBS baada ya kuambiwa na mizimu afanye hivyo.

Mtandao wa TMZ, unamnukuu mwanamuziki huyo akisema hakuwa na mpango wa kuzungumzia tuhuma zake za kuwatumikisha mabinti kingono lakini aliambiwa na mizimu yake ambayo siku zote imekuwa ikimsaidia katika kufanya maamuzi.

Katika mahojiano hayo yaliyoendeshwa na mtangazaji, Gayle King, R Kelly alikanusha kufanya makosa hayo kama yalivyo katika mashtaka 10 yanayomkabili.

R Kelly huku akilia alimwambia Gayle kuwa asingefanya upuuzi huo kwa kuwa tayari alikuwa akifuatiliwa kufuatia mashtaka aliyowahi kukumbana nayo miaka ya nyuma.

Kuhusu kukubali mahojiano hayo, amesema imempa amani kwa kuwa ametimiza alichotakiwa kufanya na haimsumbui kuona anavyozungumziwa vibaya.