Wahamiaji 39 wafariki ajali ya moto Mexico

Muktasari:

  • Wahamiaji 39 wamefariki dunia kufuatia ajali ya moto katika kituo cha wahamiaji nchini Mexico.

Mexico. Takribani wahamiaji 39 wamefariki katika ajali ya moto Jumatatu jioni katika kituo cha wahamiaji katika mji wa mpaka wa kaskazini wa Ciudad Juárez nchini Mexico.

Kwa mujibu wa taarifa ya Taasisi ya Kitaifa ya Uhamiaji (INM), wahamiaji wengine 29 walijeruhiwa katika moto huo ulioanza kabla ya saa 10 jioni katika "eneo la malazi" la kituo hicho, ambapo walipelekwa katika hospitali nne tofauti za Ciudad Juárez katika hali "dhaifu", taasisi hiyo imesema.

Jumla ya wanaume 68 wa Amerika ya Kati na Amerika Kusini walikuwa wakishikiliwa katika kituo hicho cha wahamiaji katika jiji la Chihuahua mkabala na El Paso, Texas.

Wahamiaji wote katika kituo hicho waliuawa au kujeruhiwa katika moto huo.

INM haikutaja uraia wa waathiriwa, lakini Wizara ya Mambo ya Nje  ilisema kuwa 28 kati ya waliofariki waliaminika ni kutoka nchini humo. Ofisa mmoja wa Mexico ameliambia Shirika la Habari la Reuters kwamba Wahondurasi pia walikuwa miongoni mwa waliofariki.

Rais wa Mexico López Obrador alisema Jumanne asubuhi kwamba ilionekana kuwa wahamiaji walichoma magodoro walipogundua kuwa watafukuzwa.

"Hii inahusiana na maandamano ambayo tunadhania yalianza walipogundua kwamba watafukuzwa," aliwaambia waandishi wa habari katika mkutano na wandishi Jumanne asubuhi.

"Hawakuwahi kufikiria kuwa hii ingesababisha msiba huu mbaya," alisema Obrador, ambaye alibaini kuwa wengi wa wahamiaji hao walikuwa kutoka Amerika ya Kati na Venezuela.

Kulingana na shirika la habari la eneo la Verdad Juárez, wahamiaji hao walizuiliwa siku ya Jumatatu, wakifungiwa katika kituo hicho na kutopewa chochote kwa saa kadhaa.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Guatemala amesema kuwa maofisa wa Mexico wamewafahamisha kwamba wahamiaji wa Venezuela wamechoma magodoro hayo kwa moto. Bila kutoa maelezo, INM ilisema kwamba "Inakataa kwa nguvu vitendo vilivyosababisha janga hili," amesema.

Pia ilisema kwamba iliwasilisha malalamiko kwa mamlaka husika ili kilichotokea kichunguzwe.

Shahidi aliambia Shirika la Habari la Reuters kwamba aliona miili na mifuko ya miili ikiwa imepangwa nje ya kituo hicho.

“Nilikuwa hapa tangu saa moja alasiri nikimsubiri baba wa watoto wangu na ilipofika saa 10 jioni huku na huku, moshi ukaanza kutoka kila mahali,” alisema Viangly Infante, mwanamke wa Venezuela mwenye umri wa miaka 31.

Alithibitisha kuwa moto huo ulikuwa umezimwa. Magari ya wagonjwa, zima moto na magari ya kubebea maiti ya Ciudad Juárez yaliingia katika kituo hicho, kulingana na ripoti ya Associated Press.


Imeandaliwa na Victor Tullo.