40 wauawa na Boko Haram Nigeria

Muktasari:

Hadi sasa watu wanaokadiriwa kufikia 20,000 wameuawa na   maelfu kugeuzwa mateka tangu kuibuka kwa kundi hilo mwaka 2009.

Nigeria. Zaidi ya watu 40 wameuawa wakati wa jaribio la kuwaokoa watu waliotekwa na kundi la wanamgambo wa Boko Haram nchini Nigeria.

Takriban watu watano wa kampuni ya kuchimba mafuta waliuawa, kwa mujibu wa taarifa kutoka Chuo cha Maiduguri. Wanajeshi pia waliuawa wakati wa uvamizi huo.

Idadi hiyo kubwa ya vifo ni pigo kwa Serikali ambayo inasisitiza kuwa kundi la Boko Haram limeshindwa.

Takriban watu 20,000 wameuawa na maelfu ya wengine kutekwa tangu Boko Haram ianzishe harakati zake mwaka 2009.

Katika kisa kibaya zaidi Boko Haram waliteka wasichana 276 kutoka shule ya wasichana Kaskazini Mashariki mwa Nigeria katika mji wa Chibok mwaka 2014.

Ripoti za awali kutoka kwa jeshi nchini humo zimesema kuwa waliotekwa walikuwa wakifanya kazi katika Chuo cha Maiduguri lakini baadaye waliachiwa.

Siku ya Jumanne jeshi lilisema kuwa miili ya wanajeshi tisa na raia mmoja ilipatikana.